Habari

Madiwani walilipwa Sh600 milioni Gen Z wakiandamana 2024

Na ERIC MATARA June 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KATI ya Juni 2024 na Juni 2025, wakati ambapo Wakenya walikuwa pagumu kutokana na maandamano ya Gen Z, madiwani nao walikuwa wakitia mfukoni mamilioni ya hela kupitia marupurupu.

Ripoti ya Mkaguzi wa Bajeti, Nancy Gathangu ya mwaka wa kifedha uliokamilika Juni 30, 2025, inaonyesha madiwani katika zaidi ya mabunge 17 walilipwa zaidi ya Sh600 milioni kama marupurupu ya usafiri, nyumba na marupurupu spesheli.

Ukaguzi huo unaanika malipo ya kutiliwa shaka katika kaunti za Garissa, Isiolo, Wajir, Tana River, Mandera, Samburu, Laikipia, Narok, Vihiga, Uasin Gishu, Elgeyo Marakwet, Nyandarua, Murang’a, Nyamira na Nairobi.

Katika Kaunti ya Garissa kwa mfano, madiwani 17 maalum walilipwa Sh28.3 milioni kama marupurupu.

“Walilipwa Sh147, 481 kama marupurupu ya usafiri kwa mwezi na jumla ya Sh28.3 milioni. Bunge la Kaunti halikutoa sababu ya kuwapa madiwani marupurupu hayo makubwa,” ikasema ripoti ya mkaguzi.

Isiolo haikuachwa nyuma ambapo madiwani walilipwa Sh5.7 milioni kama marupurupu ya siku nne kwa siku nne za sherehe za kumaliza kwa mwaka. Kinaya ni kwamba sherehe hiyo iliandaliwa kilomita 10 kutoka Bunge la Kaunti ya Isiolo.

“Sheria ya Tume ya Kutathmini Mishahara inasema kuwa marupurupu yanastahili kulipwa iwapo mikutano itaandaliwa kilomita 10 kutoka mahala pa kazi. Isitoshe hakukuwa na sajili ya kuonyesha idadi ya madiwani waliofika,” ikasema ripoti.

Madiwani walipokea Sh6.4 milioni kama marupurupu kwenye warsha ya siku mbili Meru na Nanyuki ila hakuna ushahidi wowote kuwa mikutano hiyo ilifanyika.

Katika Kaunti ya Laikipia, madiwani walipokea jumla ya Sh62 milioni kama marupurupu ya usafiri na kufanya vikao vya kamati.

Baada ya ukaguzi ilibainika kuwa hakukuwa na stakabadhi ambazo zilionyesha jinsi ambavyo Sh30.1 milioni zilivyolipwa.

Hali ilikuwa vivyo hivyo katika Kaunti ya Tana River ambapo madiwani walipokea Sh23.4 milioni kama marupurupu ilhali hakukuwa na ushahidi wowote kuwa malipo hayo yalitolewa.

Kiambu, wanachama wa zamani wa Bodi ya Huduma za Kaunti walilipwa Sh3.2 milioni licha ya kuwa hawakuhudhuria kikao chochote cha bodi kufikia mwisho wa mwaka wa kifedha wa 2024/2025.

Katika Kaunti ya Elgeyo Marakwet, madiwani walipokea marupurupu ya Sh134.6 milioni lakini hakukuwa na maelezo ya kuthibitisha malipo hayo.