• Nairobi
  • Last Updated March 28th, 2024 6:50 PM
Viongozi wa Jubilee wamponda Maraga, wamsifu Matiang’i

Viongozi wa Jubilee wamponda Maraga, wamsifu Matiang’i

Na PETER MBURU

VIONGOZI wa Jubilee wamemkabili vikali Jaji Mkuu David Maraga kwa kutetea majaji ambao wanadaiwa kutoa maagizo ya kuzuia shughuli za serikali, huku wakimtetea Waziri wa Usalama wa Ndani Dkt Fred Matiang’i kutokana na vita vya matamshi na Idara ya Mahakama.

Wakiongozwa na mbunge wa Gatundu Kusini Moses Kuria na Seneta wa Nakuru Bi Susan Kihika, viongozi hao walilaumu mahakama ambazo zimekuwa zikitoa amri za kuzuia maagizo ya serikali wakisema zimechangia kudorora kwa maendeleo nchini.

Viongozi hao aidha walimtetea Dkt Matiang’i kwa madai aliyotoa kuwa maafisa wa mahakama wamekuwa wakishirikiana na baadhi ya mawakili na watu wanaonuia kusambaratisha serikali.

Walikuwa wakizungumza katika hafla ya mazishi ya nduguye mbunge wa Subukia Samuel Gachobe, marehemu Ibrahim Gachobe aliyeaga dunia wiki iliyopita baada ya kuugua saratani.

“Majaji wamekuwa wakitoa maagizo kuhusu kila kitu wanachoombwa na watu wasiotaka maendeleo. Sisi kama wabunge tuko nyuma ya Bw Matiang’i na tunamrai kusimama kidete. Hatutaki kuingilia utendakazi wa idara ya mahakama lakini suala la kutoa amri za kuzuia mambo kila mara halitoi mwelekeo mwema,” akasema Bw Kuria.

Mbunge huyo alirejelea agizo lililotolewa kuzuia tume ya NTSA kufanya mafunzo ya kisasa kwa madereva, akisema inahatarisha kuongeza ajali za barabarani.
Wabunge wengine waliohudhuria ni Gabriel Kago (Githunguri), John Kiarie (Dagoretti Kusini), Kuria Kimani (Molo), Caleb Kositany (Soy), Liza Chelule (Nakuru) na Jane Njiru (Embu).

Vilevile, Gavana wa Nakuru Lee Kinyanjui, seneta wa Laikipia John Kinyua na mbunge wa EALA Mpuri Aburi walihudhuria.

iongozi hao walizidi kusema kuwa eneo la Mlima Kenya litampigia kura naibu wa rais William Ruto katika uchaguzi wa Urais 2022 na kumtaka rais kuwa makini katika uhusiano wake na aliyekuwa waziri mkuu Raila Odinga.

“Ikiwa Bw Ruto alimuunga mkono rais 2002, kisha akajiunga naye 2013 na kushirikiana naye 2017, basi watu wa Meru na Embu hatuna shaka kuwa tutamuunga mkono ifikapo 2022, hakutakuwa na njia nyingine,” akasema Bw Aburi.

Mwanasiasa huyo aidha alimtahadharisha Rais Kenyatta kujichunga anapotembea na Bw Odinga, akisema hajaamua kujiunga na serikali ila anacheza hila tu.

“Hata mnapoomba naye usifunge macho kwani tunajua kuwa hajabadilika, Raila bado ana hila zake tu,” akasema mbunge huyo.

You can share this post!

Raila hawezi kuaminika kisiasa – Gavana Waititu

Nilikuwa tu refa, Spika Lusaka ajitetea kuhusu kumng’oa...

adminleo