Chunga usisombwe na mafuriko jijini, idara yaonya
Idara ya Utabiri wa Hali ya Hewa nchini Kenya imetoa onyo la mvua kubwa, katika maeneo kadhaa ya nchi, huku jiji la Nairobi likitajwa kuwa miongoni mwa maeneo yaliyo katika hatari kubwa ya mafuriko.
Katika utabiri wake, unaohusu kipindi cha Oktoba 23 hadi Oktoba 30, wataalamu wa hali ya hewa wamesema kuwa sehemu za Bonde la Ziwa Victoria, Bonde la Ufa, na Nyanda za Juu Magharibi mwa Bonde la Ufa tayari zinaendelea kushuhudia mvua, lakini kiwango chake kinatarajiwa kuongezeka zaidi wiki ijayo.
Kulingana na Idara ya Hali ya Hewa, mvua hiyo inatarajiwa kuongezeka hadi zaidi ya milimita 30 ndani ya saa 24, na kusambaa hadi Nyanda za Juu Mashariki mwa Bonde la Ufa, ikiwemo Nairobi.
Wataalamu hao pia walisema kuwa kuanzia Oktoba 30, mvua inatarajiwa kufika maeneo ya Kaskazini Mashariki, ishara kwamba msimu wa mvua fupi za Oktoba hadi Desemba umeanza katika sehemu nyingi za nchi.
Miongoni mwa kaunti zitakazopokea mvua nyingi zaidi ni Kisumu, Homa Bay, Siaya, Migori, Busia, Kisii, Nyamira, Nandi, Kericho, Bomet, Kakamega, Vihiga, Bungoma, Narok, Baringo na Nakuru.
Kaunti nyingine ni Trans Nzoia, Uasin Gishu, Elgeyo Marakwet, West Pokot, Turkana, Isiolo, Samburu, Marsabit, Mandera, Wajir, Nyandarua, Laikipia, Nyeri, Kirinyaga, Murang’a, Kiambu, Meru, Embu, Tharaka-Nithi, Nairobi, na sehemu za Kajiado, Machakos na Makueni.
Kwa kuzingatia hali hiyo, Idara ya Hali ya Hewa imewahimiza wakazi wa maeneo yaliyoathiriwa kuwa waangalifu zaidi, kwani mvua hiyo nzito huenda zikasababisha mafuriko ya ghafla na maporomoko ya ardhi, hasa katika maeneo ya tambarare na yenye milima.
“Wakazi wa maeneo yote yaliyotajwa wanashauriwa kuwa macho dhidi ya uwezekano wa mafuriko. Maji ya mafuriko yanaweza kujitokeza hata katika sehemu ambazo hazijapokea mvua nyingi, hususan maeneo ya chini,” ilionya idara katika taarifa.
“Watu wanaoishi katika maeneo yanayokumbwa na hatari ya maporomoko ya ardhi, hususan kwenye miteremko ya Milima ya Aberdare, Mlima Kenya na maeneo yenye mteremko katika sehemu za magharibi, wanapaswa kuwa katika hali ya tahadhari,” iliongeza.
Katika jiji la Nairobi, hatari ni kubwa zaidi kutokana na mifumo duni ya kuondoa maji taka, hali inayofanya jiji kuwa katika hatari ya mafuriko.
Madereva wameonywa kutojaribu kupita maeneo yenye maji yanayotiririka au yaliyotuama, kwani hata maji madogo yanaweza kusukuma gari barabarani au kuficha mashimo yaliyo wazi.