Makala

Ngurumo za radi zaja na mvua wikendi, Idara yaonya

Na BENSON MATHEKA February 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

Kaunti ya Nairobi pamoja na maeneo ya Magharibi mwa Kenya yanatarajiwa kupokea mvua kubwa ikiambatana na ngurumo za radi mwishoni mwa wiki hii.

Idara hiyo imetaja Nairobi miongoni mwa maeneo 12 yanayotarajiwa kupata mvua ya juu ya wastani kuanzia Februari 27 hadi Machi 3, 2026. Mvua inayoambatana na radi inatarajiwa kunyesha usiku wa Ijumaa, Februari 27, asubuhi ya Jumamosi, Februari 28, na kuendelea hadi alasiri katika maeneo ya Magharibi mwa Kenya, Bonde la Ziwa Victoria, Bonde la Ufa, Nyanda za Juu za Kati na Nyanda za Chini za Kusini Mashariki.

Nairobi, iliyo katika ukanda wa Nyanda za Juu Mashariki mwa Bonde la Ufa, inatarajiwa kupokea mvua ya wastani hadi kubwa, huku kiwango kikubwa kikitabiriwa kufikia kilele Februari 28.

Zaidi ya kaunti 40 zimewekwa katika hali ya tahadhari, ikiwemo Migori, Kakamega, Nakuru, Kisumu, Kericho, Kiambu, Murang’a, Nyeri, Meru, Kajiado, Machakos, Mombasa, Kilifi na Tana River. Kaunti nyingine zilizo kwenye orodha ya uangalizi ni pamoja na Nyamira, Busia, Vihiga, Baringo, Elgeyo Marakwet, Trans Nzoia, Nandi, Uasin Gishu, Siaya, Homa Bay, Kisii, Bomet, Embu, Kirinyaga, Nyandarua, Laikipia na Tharaka-Nithi.

Maeneo ya Isiolo, Marsabit na Garissa pia yamejumuishwa, ingawa sehemu kubwa za Kaskazini Mashariki, Kaskazini Magharibi na Pwani zinatarajiwa kuwa kavu kwa kiasi kikubwa mwishoni mwa wiki. Hata hivyo, baadhi ya maeneo yanaweza kushuhudia mvua nyepesi usiku wa Ijumaa na asubuhi ya Jumamosi.

Idara ya Utabiri wa Hewa imeonya kuhusu hatari ya mafuriko, barabara kutopitika na kupungua kwa mwonekano, hasa kwa wasafiri  wanaotumia maeneo ya mabondeni yanayokumbwa na mafuriko mara kwa mara.

Wakazi katika kaunti zilizoathiriwa wametakiwa kufuatilia taarifa rasmi za hali ya hewa na kuchukua tahadhari zinazostahili kabla na wakati wa mvua kubwa.