Makala

Mvua kubwa itanyesha maeneo haya katika siku saba zijazo

Na BENSON MATHEKA February 26th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

Maeneo kadhaa yatapata mvua kubwa katika siku saba zijazo, utabiri umeonyesha.

Jiji la Nairobi ni miongoni mwa maeneo 12 yanayotarajiwa kushuhudia mvua kubwa kuliko wastani katika siku chache zijazo, kulingana na utabiri wa hivi punde wa Idara ya Utabiri wa Hewa Kenya.

Idara hiyo imetoa tahadhari ya mvua kubwa  Nairobi na maeneo mengine kadhaa, ikionya kuwa kunyesha kwa kiwango kikubwa kunatarajiwa kati ya Februari 25 na Machi 3, 2026.

Kwa mujibu wa utabiri huo, Nairobi inatazamiwa kupokea mvua ya wastani hadi kubwa, huku kiwango kikubwa kikitarajiwa kati ya Februari 25 na Februari 28.

Idara ya hali ya hewa imesema kuwa kuanzia Machi 1, kiwango cha mvua kinatarajiwa kupungua polepole katika maeneo ya Nyanda za Juu Mashariki mwa Bonde la Ufa, Nyanda za Chini Kusini Mashariki pamoja na Ukanda wa Pwani, yakiwemo maeneo ya Nairobi.

Hata hivyo, wakazi wametahadharishwa kuendelea kuwa macho kutokana na uwezekano wa mafuriko, mafuriko ya ghafla, radi na kupungua kwa mwonekano barabarani.

Maeneo yaliyotajwa kuathiriwa na mvua hii ni pamoja na Magharibi mwa Kenya, Bonde la Ziwa Victoria, Bonde la Ufa, Nyanda za Juu za Kati, sehemu za Mashariki mwa Kenya na Ukanda wa Pwani.

Kaunti zilizoorodheshwa ni Migori, Nyamira, Bungoma, Busia, Kakamega, Vihiga, West Pokot, Baringo, Elgeyo Marakwet, Trans Nzoia, Nandi, Uasin Gishu, Nakuru, Siaya, Kisumu, Homa Bay, Kisii, Kericho, Bomet, Kiambu, Embu, Murang’a, Kirinyaga, Nyandarua, Nyeri, Laikipia, Tharaka-Nithi, Meru, Narok, Kajiado, Makueni, Machakos, Taita-Taveta, Kitui, Kwale, Mombasa, Tana River, Kilifi pamoja na sehemu za Isiolo, Marsabit na Garissa.

Kwa mujibu wa utabiri huo, mvua kubwa ya zaidi ya milimita 20 ndani ya saa 24 inatarajiwa kuendelea katika Bonde la Ziwa Victoria na Nyanda za Juu Magharibi mwa Bonde la Ufa hadi Machi 3, 2026.

Wakati huo, halijoto ya juu katika maeneo hayo inatarajiwa kufikia nyuzi joto 30 Selsiasi huku kiwango cha chini kikishuka hadi nyuzi 12 Selsiasi.

Idara hiyo imeonya kuwa maji ya mafuriko yanaweza kuonekana hata katika maeneo ambayo hayajapokea mvua kubwa, hasa sehemu za chini ya mito.

Aidha, madereva wametakiwa kuwa waangalifu kutokana na barabara kuteleza na mwonekano hafifu wakati wa mvua kubwa.

Tahadhari hii inajiri wakati ambapo Nairobi imekuwa ikishuhudia mifumo isiyotabirika ya mvua, hali ambayo imekuwa ikiathiri shughuli za kiuchumi na kusababisha usumbufu mkubwa kwa wafanyakazi wanaotegemea usafiri wa umma.

Mafuriko ya ghafla katika baadhi ya maeneo ya jiji yamekuwa yakivuruga biashara na kuchelewesha shughuli za kila siku.