Makala

Chungeni mafuriko maeneo haya siku tatu zijazo,bado mvua kubwa yaja

Na BENSON MATHEKA March 4th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

Mvua kubwa inatarajiwa kuanza Jumatano hadi Jumamosi, Machi 7, 2026, hali inayoongeza hatari ya mafuriko katika kaunti nyingi nchini.

Katika tahadhari iliyotolewa Jumanne jioni, Idara ya Utabiri wa Hewa Kenya (KMD) ilionya kuwa mvua inayozidi milimita 20 itaendelea kushuhudiwa katika maeneo mengi ya nchi ndani ya saa 24.

Maeneo yatakayoathirika ni pamoja na Bonde la Ziwa Victoria, Magharibi mwa Kenya, sehemu za nyanda za juu za Kati, Bonde la Ufa na tambarare za Kusini Mashariki. Ukanda wa Pwani nao unatarajiwa kupokea mvua kubwa hadi Machi 9, 2026.

“Wakazi wa maeneo yote yaliyotajwa wanashauriwa kuwa macho dhidi ya mafuriko, mafuriko ya ghafla, kupungua kwa mwonekano na hatari nyingine zinazoweza kujitokeza,” ilisema taarifa ya KMD.

Idara hiyo ilieleza kuwa hata maeneo ambayo hayajapokea mvua kubwa yanaweza kushuhudia mafuriko, hasa yale yaliyo chini ya mito au mabonde, kutokana na maji yanayotiririka kutoka sehemu za juu. Hivyo, wakazi wametakiwa kuwa waangalifu na kufuatilia taarifa rasmi za hali ya hewa.

Kaunti zilizotajwa kuwa katika hatari ni Turkana, Samburu, Migori, Nyamira, Bungoma, Busia, Kakamega, Vihiga, West Pokot, Baringo, Elgeyo Marakwet, Trans Nzoia, Nandi, Uasin Gishu, Nakuru, Siaya, Kisumu, Homa Bay, Kisii, Kericho, Bomet, Kiambu, Embu, Murang’a, Kirinyaga, Nyandarua, Nyeri, Laikipia, Tharaka-Nithi, Meru, Nairobi, Narok, Kajiado, Makueni, Machakos, Taita-Taveta, Kitui, Kwale, Mombasa, Tana River, Kilifi, Isiolo, Marsabit, Garissa na sehemu za Wajir na Mandera.

Kiwango cha mvua kimebashiriwa kuwa cha wastani hadi kubwa, na uwezekano wa wastani kutokea katika maeneo mengi. KMD iliwashauri madereva kuepuka kuendesha magari katika barabara zilizofurika maji, ikisisitiza kuwa magari yanaweza kusombwa hata katika kina kifupi cha maji yanayotiririka kwa kasi. Watembea kwa miguu nao wamehimizwa kuepuka kuvuka mito au kutembea kwenye maji yanayotembea.

Aidha, wakazi walitahadharishwa kuepuka kujikinga chini ya miti, karibu na madirisha yenye vyuma au katika maeneo ya wazi wakati wa dhoruba ili kupunguza hatari ya kupigwa na radi.

Wiki iliyopita, wakazi kutoka sehemu mbalimbali za nchi waliripoti kushuhudia mvua kubwa, radi na ngurumo kali hasa nyakati za usiku.  KMD ilisema ongezeko la ngurumo na radi linahusishwa pakubwa na mabadiliko ya tabianchi yanayoathiri mifumo ya hali ya hewa nchini.

Alieleza kuwa hali hiyo husababisha kuongezeka kwa joto na nishati hewani, jambo linalochochea dhoruba za radi hata katika maeneo ambayo hapo awali hayakuwa yakishuhudia mvua za mara kwa mara.

Kwa mujibu wa kaimu Mkurugenzi wa KMD, Edward Muriuki, wakulima wanapaswa kuongozwa na tarehe rasmi za kuanza kwa msimu wa mvua zilizothibitishwa kisayansi katika maeneo yao badala ya kutegemea mvua ya mapema pekee.

Alionya kuwa mvua ya hivi karibuni katika baadhi ya maeneo zinaweza kuwa za mapema na si lazima ziashirie mwisho wa ukame, hasa katika maeneo kame na nusu kame ya Kaskazini na Mashariki mwa nchi ambako msimu mkuu wa mvua bado haujaanza.