• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 9:50 AM
KAULI YA MATUNDURA: Ken Walibora anavyoendeleza taswira ya uana katika ‘Mgomba Changaraweni’

KAULI YA MATUNDURA: Ken Walibora anavyoendeleza taswira ya uana katika ‘Mgomba Changaraweni’

Na BITUGI MATUNDURA

‘MGOMBA Changaraweni’ ni mojawapo ya kazi nyingi za fasihi alizotunga Ken Walibora.

Marehemu Walibora alifahamika sana kwa utunzi wa riwaya na hadithi fupi ingawa pia alichangia mno utanzu wa fasihi ya Kiswahili ya watoto.

Baadhi ya kazi zake ni pamoja na riwaya za Siku Njema (Longhorn,1996), Kufa Kuzikana (Longhorn, 2003), Ndoto ya Almasi (Moran,2007).

Vitabu vyake vya fasihi ya Kiswahili ya watoto ni pamoja na Ndoto ya Amerika (Sasa Sema, 2001) Mtu wa Mvua (Phoenix, 2004) Chapuchapu (Phoenix, 2006), Nimeshindwa Tena (Phoenix) na Mgomba Changaraweni (Phoenix) ambacho ni mojawapo ya kazi ninayoihakiki katika makala haya.

‘Mgomba Changaraweni’ ni hadithi kuwahusu jagina mchunga mifugo anayeitwa Chongameno na msichana kwa jina Alice Kesho ambaye anampenda Chongameno.

Chongameno kwa upande wake anakataa penzi la Alice. Hali hiyo inamfanya Alice kusababisha hasara na mateso makubwa kwa jamii yake kwa sababu Chongameno anakataa kumuoa. Moto aliouwasha ukateketeza msitu wa Suwerwa.

Mwanzo, jamii yake inafikiria kwamba Chongameno ndiye mhalifu aliyetenda kosa hilo na kumtumbukiza gerezani.

Mwishowe, inabainika kwamba kwa hakika Chongameno hana hatia kupitia kwenye ujumbe katika kijikaratasi alichoandika Alice kabla ya kujiua.

Hadithi hii ina sifa za vitabu vya fasihi ya watoto tulizotaja katika sura ya pili.

Ina sura fupi, ni sahili na inasomeka kwa urahisi. Aidha, ina michoro na imechapwa kwa maandishi makubwa na lugha sahili.

Taswira dumifu za uana katika ‘Mgomba Changaraweni’ zinadhihirika hasa tunapoangazia hulka ya wahusika wakuu katika hadithi hii na majukumu yao ya kikazi.

Chongameno ambaye ni mhusika mkuu na wa jinsia ya kiume amesawiriwa kama kijana mwenye nguvu aliyefanya kazi za ushokoa bila kuchoka.

Picha ya Chongameno inayojitokeza katika hadithi hii inaendeleza taswira dumifu katika jamii kwamba mwanamume ni kiumbe mwenye nguvu na uwezo mkubwa wa kutenda mambo anapolinganishwa na mwanamke.

Alice Kesho kwa upande mwingine amesawiriwa kama kiumbe mrembo na safi anayependa kujirembesha kila wakati. Tunafahamishwa: Alisimama wima mbele ya kioo chake, kifua wazi alivyozaliwa. Aliyatazama kiooni madodo yake akayaona yameiva. Akacheka.

“Nani kama mimi?” akajisemea.

Akajipaka mafuta mwilini. Ngozi yake ilikuwa laini. Hakuzoea kazi ya sulubu kama vijakazi wa pale nyumbani, waliojisaga kazini kama watumwa hasa.

Haikuwa ajabu basi kuwa ngozi yake ilikuwa laini na nyororo. Alikuwa na umbo la wastani, si mwembamba sana si mnene sana, na ngozi yake ya maji ya kunde iliwapa vijana wavulana pumbao na tamanisho (Uk. 19).

Hulka ya Alice Kesho kuwa mtegemezi wa Chongameno inajitokeza mwishoni mwa hadithi hasa anapoamua kujiua kwa sababu haoni maana ya maisha baada ya Chongameno kukataa ombi lake la kumtaka awe mpenzi wake.

Hatua ya kujiua inazua maswali mengi kuliko majibu. Je, kulikuwa na haja ya Alice Kesho kujiua?

Hatua hiyo inaonyesha kwa vyovyote udhaifu alio nao mwanamke kutoweza kuishi bila kumtegemea mwanamume?

(Makala yataendelea)

[email protected]

You can share this post!

Serge Aurier ajiunga na Villarreal ya Uhispania

USWAHILINI: Turathi ya Misitu ya Kaya na manufaa yake kwa...