• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 8:50 AM
Italia waponda Jamhuri ya Czech kirafiki na kuvuna ushindi wa nane mfululizo bila kufungwa bao

Italia waponda Jamhuri ya Czech kirafiki na kuvuna ushindi wa nane mfululizo bila kufungwa bao

Na MASHIRIKA

TIMU ya taifa ya Italia ilipokeza Jamhuri ya Czech kichapo cha 4-0 katika mechi ya kirafiki iliyochezewa mjini Bologna mnamo Ijumaa usiku.

Mchuano huo ulikuwa wa nane mfululizo kwa Italia kushinda bila kufungwa bao.

Ciro Immobile aliwafungulia Italia karamu ya mabao katika dakika ya 23 kabla ya Nicolo Barella kupachika wavuni goli la pili mwishoni mwa kipindi cha kwanza.

Lorenzo Insigne aliyekuwa akiadhimisha miaka 30 ya kuzaliwa alifunga bao la tatu la Italia kunako dakika ya 66 kabla ya Domenico Berardi kuzamisha kabisa chombo cha Jamhuri ya Czech katika dakika ya 73.

Chipukizi Giacomo Raspadori, 21, ambaye anacheza pamoja na Berardi kambini mwa Sassuolo katika Ligi Kuu ya Italia (Serie A), aliletwa ugani katika dakika ya 78.

Chini ya kocha Roberto Mancini, Italia hawajapoteza mchuano wowote tangu 2018. Mabingwa hao wa Kombe la Dunia 2006 watafungua rasmi kampeni zao za Euro mnamo Juni 11 dhidi ya Uturuki.

Italia na Uturuki wametiwa katika Kundi A kwa pamoja na Wales na Uswisi. Kwa upande wao, Jamhuri ya Czech iko katika Kundi D kwa pamoja na Uingereza, Scotland na Croatia ambao walikuwa wanafainali wa Kombe la Dunia mnamo 2018 nchini Urusi.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Mkenya Mudibo achaguliwa naibu rais wa tenisi ya mezani...

Demu afumaniwa akiroga wakwe