• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:55 AM
UDAKU: Kibibi Jocelyn Burgardt anavyomkimbiza Cavani polo hatulii Old Trafford

UDAKU: Kibibi Jocelyn Burgardt anavyomkimbiza Cavani polo hatulii Old Trafford

Na CHRIS ADUNGO

UJAUZITO wa Jocelyn Burgardt, ambaye ni mchumba wa Edison Cavani, ni miongoni mwa sababu zitakazomchochea straika huyo wa Uruguay kuondoka Manchester United na kurejea Amerika Kusini mwishoni mwa msimu huu wa 2020-21.

Gazeti la Infobae nchini Argentina limedai kwamba refa wa mahaba yuko karibu kuhesabu bao la kimapenzi ambalo Jocelyn, 29, alifungwa na Cavani, 34, miezi sita iliyopita.

Kupitia mtandao wake wa Instagram, kipusa huyo amesema angetamani sana Cavani awe karibu naye wanavyozidi kumsubiri mtoto wao wa pili azaliwe mwezi Juni.

Zaidi ya kuathiriwa na hali mbaya ya hewa jijini Manchester, Uingereza, kingine ambacho kitakuwa kiini cha Cavani kugura Man-United ni hamu ya kuungana na beki wa zamani wa timu hiyo, Marcos Rojo, aliye kambini mwa Boca Juniors nchini Argentina.

“Nilikutana na Cavani nchini Uruguay mwezi uliopita na akaniambia nimsubiri Boca Juniors kuanzia Juni,” akasema Rojo.

“Isitoshe, bado ana machungu ya kupigwa marufuku mechi tatu pamoja na faini ya Sh14 milioni kwa kutumia neno ‘negrito’ mtandaoni, lililofasiriwa na Shirikisho la Soka Uingereza (FA) kuwa la kiuchochezi na matusi,” akaongeza Rojo.

“Muhimu zaidi, hata hivyo, ni kwamba mpenzi wake ni mjamzito na tayari amerejea Uruguay. Cavani atataka sana kuwa naye ili amwondolee kijibaridi cha upweke anaposubiri kuangusha toto,” alifafanua beki huyo.

Japo inasuburiwa Cavani kurefusha mkataba wake ugani Old Trafford, sogora huyo wa zamani wa Paris Saint-Germain (PSG) anatamani sana kuwa karibu na familia yake.

Kufikia sasa, Cavani ana watoto watatu baada ya uhusiano wake na Jocelyn kujaliwa binti kwa jina India mnamo Mei 2019.

Mvamizi huyo matata pia aliwahi kupata vidume viwili – Bautista na Lucas – katika uhusiano na kidosho Maria Soledad.

Mnamo Oktoba 2020, Cavani alifichua kwamba nusura astaafu kabisa soka, baada ya yeye na mchumba wake Jocelyn kupata virusi vya corona wakiwa likizoni kwenye ufuo wa Ibiza nchini Uhispania.

Wakiwa huko, walitangamana na wanasoka wa PSG – Angel de Maria na Mauro Icardi ambao pia waliugua Covid-19.

Jocelyn alianza kutoka kimapenzi na Cavani mnamo 2014, miezi michache baada ya sogora huyo kutemana na Soledad sababu ya jicho kali la nje; lililomfanya fowadi huyo wa zamani wa Napoli kuanza kumtambalia mwanahabari wa Italia, Maria Rosario.

Uhusiano kati ya Cavani na Rosario ulidumu kwa miezi tisa pekee baada ya Rosario kudai kwamba mwanasoka huyo ana wivu na asingemtaka kabisa atangamane na marafiki zake. Aliyemkutanisha Cavani na mpenzi wake wa sasa ni mwanasoka matata wa Uruguay, Gaston Ramirez.

Mnamo Oktoba 2020, Cavani alifichua kwamba nusura astaafu kabisa kwenye ulingo wa soka baada ya yeye na mchumba wake Jocelyn kupata virusi vya corona walipokuwa likizoni, kwenye ufuo wa Ibiza nchini Uhispania. Wakiwa huko, walitangamana na wanasoka wa PSG – Angel de Maria na Mauro Icardi ambao pia waliugua Covid-19.

You can share this post!

Pigo Ruto akipoteza ‘jenerali’

Usalama waimarishwa katika mpaka wa Kenya na Somalia...