• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 10:50 AM
Anayedaiwa kujaribu kuua Kosewe ‘atikisa’ kesi

Anayedaiwa kujaribu kuua Kosewe ‘atikisa’ kesi

Na RICHARD MUNGUTI

UAMUZI wa kesi ya jaribio la kumuua mmiliki wa hoteli ya Ranalo almaarufu Kosewe uliyumbisha kuhukumiwa kwake alipowasilisha ombi akubaliwe kuita mashahidi zaidi kabla ya kuhukumiwa.

Bw Tom Oywa Mboya alifika mbele ya hakimu mkuu wa mahakama ya Milimani, Bi Martha Mutuku na kuomba apewe muda awaite mashahidi wanne zaidi kabla ya kujua hatima yake.

Lakini Bi Mutuku alimfahamisha Bw Mboya kwamba tayari ametayarisha uamuzi na yuko tayari kuusoma.

Endapo Bw Mboya atapatikana na hatia, Bw Mboya atasukumiwa kifungo cha maisha gerezani kwa kujaribu kumuua Bw Osewe, anayemiliki hoteli ya K’Osewe iliyoko katikati mwa jiji la Nairobi maarufu kwa kuandaa mlo mtamu wa samaki.

Ushahidi uliowasilishwa kortini ulibaini kuwa mshtakiwa alimpiga Bw Osewe risasi kwa sababu ya mwanamke.

Ombi hili la Bw Mboya kupitia kwa wakili Benjamin Makokha lilishangaza kiongozi wa mashtaka Bw Anderson Gikunda aliyesema “hii ni mbinu ya kuchelewesha haki kutendeka.”

Bw Gikunda aliomba korti itupilie mbali ombi hilo la mshtakiwa akisema “alibadilisha fikra baada ya kuona ushahidi uliotolewa dhidi yake umethibitisha kuwa alikuwa na nia ya kumuua Osewe”.

Bw Makokha anayemtetea mshtakiwa huyu pamoja na wakili mwenye tajriba ya juu Prof Tom Ojienda aliomba mahakama imruhusu mshtakiwa awasilishe ushahidi aliosema “utasaidia mahakama kufikia uamuzi wa haki”.

Bw Makokha alisema mshtakiwa haogopi kusomewa hukumu lakini akaomba korti izingatie maamuzi ya hapo awali ambapo upande wa mashtaka uliwasilisha ushahidi zaidi hata baada ya kufunga kesi.

Mahakama itatoa uamuzi Septemba 27, 2021 ikiwa itamruhusu mshtakiwa kuwasilisha ushahidi zaidi ama itasoma uamuzi wake.

Bw Mboya amekanusha shtaka la kujaribu kumuua Osewe katika mtaa wa Garden Estate.

Yuko nje kwa dhamana.

You can share this post!

KIKOLEZO: Kapochi ka Tik ToK

TAHARIRI: Midahalo endelevu itachochea ustawi