• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 9:50 AM
MCK yalaani mauaji katili ya mwanahabari wa KBC

MCK yalaani mauaji katili ya mwanahabari wa KBC

WANDERI KAMAU na VINCENT ACHUKA

BARAZA la Vyombo vya Habari (MCK) jana limekashifu vikali mauaji ya kikatili dhidi ya Bi Betty Barasa, aliyehudumu kama mhariri wa video katika Shirika la Utangazaji la KBC.

Kulingana na taarifa za polisi, Bi Barasa aliuawa na majambazi mnamo Jumatano usiku nyumbani kwake katika eneo la Ololulua, Ngong, Kaunti ya Kajiado, alipongojea kufunguliwa lango ili kuingia.

Aliuawa na wanaume watatu waliobeba silaha kali.

Polisi waliiambia Taifa Leo kwamba wanashuku watatu hao walikuwa wamejificha katika nyumba ya karibu na kwake, ambayo bado inaendelea kujengwa.

Alifika kwenye lango la makazi yake mwendo wa saa mbili na unusu. Baada ya kumkabili mwanahabari huyo, majambazi hao waliingia kwa nguvu nyumbani kwake na kuanza kuitisha pesa.

Wezi hao waliwashinda nguvu mumewe, mwanawe na mfanyakazi wao wa nyumba.

Kwa wakati mmoja, mmoja wa majambazi hao alimlazimu Bi Barasa kuwapeleka kwenye ghorofa ya juu kutafuta pesa walizokosa.

Walipokosa pesa, walimpiga risasi mara mbili kichwani ambapo alifariki papo hapo.

Kufuatia mauaji hayo, MCK ilikashifu mauaji hayo, huku ikiwaomba polisi kuharakisha uchunguzi ili kubaini waliohusika.

Kwenye taarifa, Afisa Mkuu Mtendaji wa baraza hilo, Bw David Omwoyo alilalamikia ongezeko la visa vya mauaji dhidi ya wanahabari katika siku za hivi karibuni.

Mwaka uliopita, mwili wa mwanahabari maarufu na mwandishi wa vitabu, Prof Ken Walibora ulipatikana katika mochari ya Hospitali Kuu ya Kenyatta (KNH) baada yake kukosekana kwa siku kadhaa.

Polisi walisema Prof Walibora aliuawa na watu wasiojulikana katika barabara ya Landhies, Nairobi.

Mwezi uliopita, aliyekuwa afisa wa mawasiliano katika Wizara ya Ardhi, Bi Jennifer Wambua, alipatikana ameuawa na mwili wake kutupwa katika msitu wa Ngong.

You can share this post!

Raila amtumia Ruto ujumbe wa muungano

Viongozi wasifu wakazi wa Garissa kwa urithi wa Haji