• Nairobi
  • Last Updated May 9th, 2024 10:18 AM
VYAMA VYA KISWAHILI: Chama cha Kiswahili katika shule ya upili ya wavulana ya Mukaa (CHAKIMU)

VYAMA VYA KISWAHILI: Chama cha Kiswahili katika shule ya upili ya wavulana ya Mukaa (CHAKIMU)

Na CHRIS ADUNGO

CHAKIMU ni chama kinachochangia matumizi bora ya Kiswahili katika Shule ya Upili ya Mukaa Boys’ iliyoko viungani mwa mji wa Salama, Kaunti ya Makueni.

Chama hiki kiko chini ya Idara ya Lugha inayoshughulikia Kiswahili na Kiingereza katika Shule ya Upili ya Mukaa.

Mwalimu Mkuu, Bw M. Tuke huhakikisha kuwa magazeti ya ‘Taifa Leo’ yamesomwa na wanafunzi wote kila siku. Pia anawanunulia vitabu vya kudurusu ili kuboresha matokeo ya somo la Kiswahili katika Mtihani wa Kitaifa wa Kidato cha Nne (KCSE).

Kwa mujibu wa Bw Deon Musau ambaye ni mlezi wa CHAKIMU, wanafunzi wake hudumisha umahiri wao katika Kiswahili kwa kujizolea alama nzuri katika mitihani ya KCSE. Siri ya mafanikio yao ni mazoea ya kusoma magazeti ya ‘Taifa Leo’ kila siku.

Isitoshe, lugha sanifu itumiwayo katika uandishi wa habari na makala katika gazeti la ‘Taifa Leo’ huwanufaisha sana wanafunzi. Wanachama huangazia masuala mbalimbali ya Kiswahili yaliyo na faida darasani na nje ya darasa.

Kufikia sasa, idadi ya wanachama wote ni mia nne. Watahiniwa wa KCSE ambao huwa wanachama wa CHAKIMU wameendeleza desturi ya kusajili matokeo bora zaidi katika somo la Kiswahili.

CHAKIMU kina vitengo mbalimbali vinavyosaidia wanachama umilisi wao katika Kiswahili. Vitengo hivyo ni pamoja na: kitengo cha ushairi, kitengo cha sanaa na uigizaji, kitengo cha sarufi, kitengo cha utangazaji na kitengo cha tafsiri na ukalimani.

Wanachama wengi huishia kutambua talanta zao kutokana na uwepo wa vitengo hivi kwa sababu madhumuni ya chama ni kuwapa wanafunzi jukwaa mwafaka la kukuza vipaji vyao vya utambaji wa hadithi, uchoraji, uigizaji, uanahabari na utunzi wa mashairi.

Chama kina wawakilishi kutoka kila kidato wakiongozwa na Calvin Mutoko (Mwenyekiti), Michael Muoki (Naibu Mwenyekiti), Abraham Kisua (Mhazini), Peter Njoroge (Mwakilishi wa Kidato cha Nne), Collins Kyengo (Mwakilishi wa Kidato cha Tatu), Geoffrey Kimeu (Mwakilishi Kidato cha Pili) na Daniel Mui (Msimamizi kitengo cha sarufi).

Chama huandaa vikao vya mara kwa mara kwa lengo la kuwashirikisha wanafunzi kikamilifu katika mashindano yanayolenga kubaini upekee wa talanta zao.

Chama kinapania pia kushiriki na kuchangia mijadala ya kitaaluma kuhusu Kiswahili kupitia vipindi vya lugha ambavyo huendeshwa katika vituo mbalimbali vya redio na runinga za humu nchini.

Kuwepo kwa CHAKIMU kumeamsha ari ya mapenzi ya Kiswahili miongoni mwa wanachama ambao kwa sasa ni mabalozi halisi wa Kiswahili na wasomaji wakubwa wa gazeti la ‘Taifa Leo‘ katika Shule ya Upili ya Mukaa Boys.

Bw Musau anaamini kuwa chama hiki kitawabadilisha wanafunzi wengi na kuwapa uwanja mpana wa kuzamia taaluma zinazohusiana na Kiswahili katika siku za usoni.

You can share this post!

Vyombo vya habari vyatakiwa kuangazia habari za kilimo cha...

ODM haitambui PAA, asema Mbunge