• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 9:50 AM
UMBEA: Mwanamke huridhishwa zaidi na ukarimu na upendo wa mwenzake

UMBEA: Mwanamke huridhishwa zaidi na ukarimu na upendo wa mwenzake

NA SHANGAZI SIZARINA

Ipo dhana kwa baadhi ya wanaume kwamba ili umpate mwanamke ama msichana ni muhimu kutunisha msuli wa pesa. Kwamba usambaze noti ili kuimarisha heshima kwa mwanamke ama msichana ambaye anakuvutia.

Imani yao kubwa ikiwa ni kwamba kawaida wanawake hupenda hela, hivyo ili kumpata kwa urahisi muonyeshe kwamba unazo hizo hela.

Mtazamo huu wa baadhi ya wanaume kwamba mwanamke analainishwa na pesa umeleta changamoto nyingi katika mahusiano na ndoa. Kwani baadhi wanadhani unapotimiza haja za mwanamke kifedha inatosha kabisa na hakuna umuhimu wa kutimiza haja zake zingine ambazo ni za kimwili ama kihisia.

Mwenendo huu huleta upweke kwa baadhi ya wanawake wanaojikuta wana kila kitu nyumbani kinachohusiana na mahitaji ya pesa, lakini wanakosa kutimiziwa mahitaji ya kihisia ama kimwili na hao wenzao. Upweke huzaa migogoro isiyokwisha ambayo huweza kufanya baadhi ya wanaume washindwe kuwaelewa wanawake. Kwa tathmini na uamuzi wao, unaweza kuona kwamba ni vigumu kumridhisha mwanamke.

Lakini wanachosahau wanaume wenye mtizamo huu ni kuwa mwanamke kwa asili yake anayo mahitaji ya msingi ambayo yanapopuuzwa, chochote kinachofanyika kama mbadala wa mahitaji hayo hakiwezi kuwa na maana yoyote. Usipoweza kujua mahitaji yake halisi, unaweza kumpa chochote kile unachodhani anakihitaji na bado mambo yasiende kama ulivyotarajia.

Pamoja na hivyo, wapo wanawake ambao lengo kubwa ni kujipatia pesa za mwanaume. Hawa ni wanawake wanaofanya biashara ya mahusiano.

Kwao, hakuna sababu yoyote ya kuwa na uhusiano imara na wenzao isipokuwa mpangilio wa kujipatia vitu na fedha. Hatuzungumzii uhusiano huo wa kibiashara kati ya mwanamume na mwanamke bali uhusiano wa dhati unaojengwa katika misingi ya upendo, uaminifu, kuelewana na ahadi ya kuwa pamoja katika dhiki na raha.

Katika hali halisi, pamoja na fedha, mwanamke huridhishwa zaidi na ukaribu na upendo wa mwenzake.

Mwanamke anahitaji kuambiwa kila mara na kuthibitishiwa kwa vitendo kuwa anapendwa. Hata hivyo, lugha ya mapenzi hutegemea mambo mengi. Kuna athari za utamaduni, desturi na imani zilizopo katika jamii aliyokulia mwanamke. Hata hivyo, yapo matendo yaliyothibitika kuvuka mipaka ya kiutamaduni.

Uelewe kwamba kuna nguvu kubwa kumwambia mwanamke unampenda, na isiwe mara moja bali mara nyingi iwezekanavyo.

Pamoja na kumpenda, mwanamke anahitaji kupata muda wa kutosha na ampendaye, ikiwezekana kutoka naye, kuwa naye nyumbani mara kwa mara pale inapowezekana. Iwapo unataka kuugusa moyo wa mwanamke, akupe heshima unayoihitaji, unawajibika kujua vitu gani mahususi ukimfanyia vinatuma ujumbe wa wazi kuwa unampenda.

Usipoweza kumfanya mwanamke ajisikie kupendwa, anapoteza hamu ya uhusiano. Huchoka kihisia na anaweza kufanya mambo yasiyotarajiwa ili tu kuhujumu mahusiano.

Pamoja na yote, mwanamke hupenda aonekane ni kipaumbele kwa mumewe. Kwamba katika hali ama hatua yeyote, mumewe anampatia kipaumbele kabla ya kufikiria ama kutenda jambo lingine. Kila la heri katika kuboresha mahusiano yako.

[email protected]

You can share this post!

MWANAMUME KAMILI: Kila nyumba huwaka moto, muhimu kujenga...

Dai serikali ilihadaa kuhusu miradi Boni