• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 6:50 AM
WARUI: Wazazi watumie fursa ya likizo kunasihi watoto wao

WARUI: Wazazi watumie fursa ya likizo kunasihi watoto wao

Na WANTO WARUI

VISA vya utovu wa nidhamu na vile vya wanafunzi kutaka kujitoa uhai vimekuwa vingi sana siku hizi.

Huku visa vya kujitoa uhai kwa watu wazima vinasababishwa na mambo mawili makuu: umaskini na mapenzi, kwa wanafunzi huenda ni matatizo tofauti kabisa.

Baadhi ya mambo yanayopelekea wanafunzi kujipata katika hali hizi mbaya ni pamoja na kujiunga na vikundi vya marafiki wabaya, kujiingiza katika matumizi ya dawa za kulevya, kutokuwa na kazi maalum nyumbani na zaidi ni kukosa ushauri nasaha kutoka kwa wazazi wao.

Wanafunzi wengi hasa walio katika shule za malazi huwa na muda mfupi sana wa likizo wa kuwa na wazazi wao.

Kuna wale wazazi ambao huwa wanaenda kazini asubuhi na mapema kisha kurudi jioni au usiku kabisa.

Hawa hawapati muda mwafaka wa kuweza kuzisoma tabia za wana wao hasa zile geni.

Wanafunzi wanapokuwa pamoja hushiriki katika mambo tofauti shuleni au popote pale walipo.

Kuna mambo mema na mengine yasiyo mema ambayo huwa wanajadiliana.

Miongoni mwa wanafunzi hao, kuna wale huathirika na mambo mabaya na hatimaye kujipata wakiyatenda.

Haya ni pamoja na kujikuta wakianza kutumia dawa za kulevya, kutazama filamu mbaya ama hata kujiingiza katika mapenzi ya kiholela.

Ni jukumu la kila mzazi kuweza kutenga muda maalum ili ajadiliane na mwanawe kuhusu mambo ambayo yanaweza kumharibia maisha yake ya baadaye.

Kwa mfano, mwanafunzi anaporudi nyuma katika matokeo yake ya masomo mwisho wa muhula, haitoshi tu mzazi kuambiwa kuwa mtihani ulikuwa mgumu.

Kuna sababu nyingi tu ambazo husababisha matokeo mabaya kwa mwanafunzi.

Baadhi ya mambo ya utovu wa nidhamu yanaweza kuonekana madogo tu na kupuuziliwa mbali hatimaye yawe mwiba usiong’oleka.Hii ndiyo sabau wazazi wanastahili kuwa macho sana na yale yote yanayoendelea katika maisha ya wana wao.

Wakati mwingine visa vya utovu wa nidhamu vinaweza kuibuka kutoka shuleni.

Endapo tabia mbaya zipo shuleni na hazijakabiliwa na uongozi wa shule ipasavyo, patakuwa na uwezekano mkubwa zikaenea hata kwa wale wanafunzi wazuri wasio na kinga ya ushauri kutoka kwa wazazi.

Ni muhimu sana kwa kila mzazi ambaye ana mtoto shuleni kuchukua fursa hii ya likizo aweze kumhoji mwanawe na kuchunguza kama ameingilia mienendo isiyofaa ili kama atagundua mambo yasiyofaa kwa mtoto aweze kukabiliana nayo mapema.

Matatizo mengi yanayowapata watoto siku za baadaye hutokana na wazazi kukosa kurekebisha makosa madogo madogo mapema yanapojitokeza nyumbani ama kukosa muda wa kujadiliana na watoto ili wawajue vyema.

Bila shaka usipoziba ufa utajenga ukuta.

You can share this post!

Watford wamfuta kazi kocha Xisco Munoz

TAHARIRI: Vijana wajisajili wasikike 2022