• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 6:50 AM
AS Roma ya kocha Jose Mourinho yapepeta Udinese na kuingia nne-bora Serie A

AS Roma ya kocha Jose Mourinho yapepeta Udinese na kuingia nne-bora Serie A

Na CHRIS ADUNGO

KIKOSI cha AS Roma sasa kinashikilia nafasi ya nne kwenye msimamo wa jedwali la Ligi Kuu ya Italia (Serie A) baada ya kupepeta Udinese 1-0 mnamo Alhamisi usiku.

Bao la pekee na la ushindi kwa upande wa Roma wanaotiwa makali na kocha Jose Mourinho lilifumwa wavuni na fowadi wa zamani wa Chelsea, Tammy Abraham katika dakika ya 36.

Roma ambao kwa sasa wanajivunia alama 12 kutokana na mechi tano zilizopita, walikamilisha mchuano huo wakiwa na wachezaji 10 pekee uwanjani baada ya Lorenzo Pellegrini kuonyeshwa kadi nyekundu mwishoni mwa kipindi cha pili.

Ni pengo la alama tatu kwa sasa ndilo linatenganisha Roma na viongozi wa jedwali Napoli waliowapokeza Sampdoria kichapo cha 4-0 katika mchuano mwingine wa Alhamisi usiku.

AC Milan na mabingwa watetezi Inter Milan ambao pia hawajapoteza mechi yoyote ligini kufikia sasa, wanajivunia alama 13 kila mmoja na wanakamata nafasi za pili na tatu mtawalia.

Inter waliwacharaza Fiorentina 3-1 ugenini huku Milan wakizamisha chombo cha limbukeni Venezia 2-0. Abraham aliyejiunga na Roma kwa Sh5.3 bilioni mnamo Agosti 2021, sasa amefungia waajiri wake wapya mabao matatu kutokana na mechi saba za mashindano yote. Mawili kati ya magoli hayo yametokana na mechi tano za Serie A.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

TAHARIRI: Midahalo endelevu itachochea ustawi

Wakazi wafurahia hatua ya Rais Kenyatta kupandisha hadhi...