• Nairobi
  • Last Updated May 10th, 2024 11:36 AM
Barcelona wapepeta Dynamo Kyiv na kunusia hatua ya 16-bora UEFA

Barcelona wapepeta Dynamo Kyiv na kunusia hatua ya 16-bora UEFA

Na MASHIRIKA

BARCELONA walisajili ushindi muhimu wa 1-0 dhidi ya Dynamo Kyvi katika gozi la Kundi E kwenye Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) mnamo Jumanne usiku nchini Ukraine.

Ushindi huo wa Barcelona uliwapaisha hadi nafasi ya pili kundini kwa alama sita, sita nyuma ya viongozi Bayern Munich.

Fowadi chipukizi Ansu Fati alifunga bao la pekee katika mchuano huo katika dakika ya 70 baada ya mpira kutokana na krosi ya Oscar Mingueza kuangukia miguuni pake.

Kyiv walipoteza nafasi nyingi za kufunga kupitia Mykola Shaparenko aliyepaisha makombora mawili licha ya kujipata pazuri zaidi kurejesha waajiri wake mchezoni.

Chini ya kocha Ronald Koeman aliyefutwa kazi kwa matokeo duni, Barcelona walifungua kampeni zao za UEFA msimu huu kwa kupoteza mara mbili kwa 3-0 dhidi ya Bayern Munich na Benfica ambao sasa wanakamata nafasi ya tatu kwa alama nne.

Mechi dhidi ya Kyvi ilikuwa ya kwanza kwa Barcelona kutandaza tangu waagane na Koeman wiki iliyopita naye kocha wa Barcelona B, Sergi Barjuan akaaminiwa kuwa mshikilizi wa mikoba ya miamba hao wa Uhispania.

Bayern wametinga hatua ya 16-bora ya UEFA kwa kipindi cha misimu 17 iliyopita mfululizo na watafuzu kwa hatua hiyo kwa mara nyingine iwapo watawakomoa Benfica mnamo Novemba 23 ugani Camp Nou.

Iwapo watazamishwa katika mechi hiyo, itamaanisha kwamba watalazimika kushinda Bayern ugenini na kutumainia kwamba Benfica watapoteza alama muhimu dhidi ya Kyiv katika raundi ya mwisho ya mechi za makundi.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Lewandowski aongoza Bayern kuzamisha Benfica na kufuzu kwa...

Riadha za Nusu-Marathon Duniani 2022 zaahirishwa kwa miezi...

T L