• Nairobi
  • Last Updated May 20th, 2024 9:16 PM
Riadha za Nusu-Marathon Duniani 2022 zaahirishwa kwa miezi tisa kwa sababu ya corona nchini Uchina

Riadha za Nusu-Marathon Duniani 2022 zaahirishwa kwa miezi tisa kwa sababu ya corona nchini Uchina

Na GEOFFREY ANENE

RIADHA za Dunia za mbio za mita 21 zimeahirishwa kutoka Machi 27, 2022 hadi Novemba 13, 2022 kwa sababu za kiusalama na masharti magumu ya usafiri ya kudhibiti maambukizi ya virusi vya corona nchini Uchina.

Shirikisho la Riadha Duniani limetangaza hayo mnamo Novemba 3, 2021 likisema kuwa limefanya mazungumzo na Kamati Andalizi ya mbio hizo na kuafikiana kuchukua hatua hiyo.

“Shirikisho la Riadha Duniani na Kamati Andalizi ya Riadha za Dunia za Nusu-Marathon zimekubaliana kuahirisha mashindano hayo yaliyofaa kufanyika mjini Yangzhou nchini Uchina mnamo Machi 27, 2022.

Sasa, yataandaliwa Novemba 13, 2022,” shirikisho hilo limesema.

Katika makala yaliyopita, Mkenya Peres Jepchirchir alitwaa taji la kinadada kwa muda uliokuwa rekodi ya dunia wa saa 1:05:16 akifuatiwa na Mjerumani Melat Yisaka (1:05:18) na Muethiopia Yalemzerf Yehualaw (1:05:19) mjini Gdynia, Poland mnamo Oktoba 17, 2020.

Mkenya Kibiwott Kandie aliridhika na nafasi ya pili katika kitengo cha wanaume kwa dakika 58:54, sekunde 0.06 nyuma ya mshindi Jacob Kiplimo kutoka Uganda naye Muethiopia Amedework Walelegn akafunga mduara wa tatu-bora.

Kenya ilishinda taji la timu za wanaume kwa jumla ya saa 2:58:10 baada ya Leonard Barsoton, Benard Kimeli na Benard Ng’eno kukamata nafasi ya sita, tisa na 42, mtawalia.

Iliridhika na nafasi ya pili nyuma ya Ethiopia kwa timu za kinadada baada ya Joyciline Jepkosgei, Brillian Jepkorir, Rosemary Wanjiru na Dorcas Jepchumba kukamilisha katika nafasi ya sita, tisa, 10 na 11, mtawalia.

  • Tags

You can share this post!

Barcelona wapepeta Dynamo Kyiv na kunusia hatua ya 16-bora...

GWIJI WA WIKI: Silvester Makau

T L