• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 5:50 AM
Bayern Munich warefusha mkataba wa fowadi Maxim Choupo-Moting kwa miaka miwili zaidi

Bayern Munich warefusha mkataba wa fowadi Maxim Choupo-Moting kwa miaka miwili zaidi

Na MASHIRIKA

BAYERN Munich wamerefusha mkataba wa fowadi matata raia wa Cameroon, Eric Maxim Choupo-Moting, 32, kwa miaka miwili zaidi.

Mkataba wa mshambuliaji huyo ambaye amekuwa akiwajibishwa mara kwa mara katika nafasi ya Robert Lewandowski, ulikuwa utamatike ugani Allianz Arena mwishoni mwa Juni 30, 2021.

Choupo-Moting aliyekuwa akivalia jezi za Stoke City miaka mitatu iliyopita, alifungia Bayern jumla ya mabao tisa kutokana na mechi 32 za msimu uliopita wa 2020-21 kwenye mapambano yote. Mchango wake ulisaidia Bayern kutia kapuni taji la Bundesliga kwa mara ya tisa mfululizo msimu huo.

Lewandowski alipopata jeraha baya la goti lililomweka nje kwa kipindi kirefu mnamo Aprili 2021, Choupo-Moting alitegemewa zaidi katika mechi mbili za robo-fainali za Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) dhidi ya waajiri wake wa zamani Paris Saint-Germain (PSG) ya Ufaransa mnamo 2020-21. Choupo-Moting alifunga bao katika mojawapo ya mechi hizo za mikondo miwili.

Bayern wataanza kampeni za msimu mpya wa 2021-22 wakijivunia huduma za Oliver Kahn akiwa mwenyekiti mpya naye Julian Nagelsmann akiwa kocha wao mpya.

Nageslmann alitokea RB Leipzig ya Ujerumani mwishoni mwa msimu wa 2020-21 kujaza pengo la Hansi Flick atakayekuwa mrithi wa Joachim Loew katika timu ya taifa ya Ujerumani kuanzia Julai 2021.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Suleiman Shahbal aahidi kuwatatulia wafanyabiashara kero...

Serikali kujenga daraja la Sh25 milioni kuokoa biashara za...