Na MASHIRIKA
BEKI wa Manchester City, John Stones, ametia saini mkataba mpya wa miaka mitano uwanjani Etihad.
Hadi aliporefusha muda wa kuhudumu kwake kambini mwa miamba hao wa soka ya Uingereza, kandarasi kati ya Stones na Man-City ilitazamiwa kutamatika rasmi mwishoni mwa mwaka wa 2022.
Stones, 27, alianza kuwa tegemeo katika kikosi cha kwanza cha Man-City mnamo 2020-21 na akawa sehemu ya kikosi kilichowajibishwa na Uingereza kwenye fainali ya Euro 2020 dhidi ya Italia uwanjani Wembley mnamo Julai 11, 2021.
Stones alitarajiwa kuondoka kambini mwa Man-City mwishoni mwa msimu wa 2020-21 baada ya mabeki Aymeric Laporte na Ruben Dias kuridhisha zaidi muhula huo.
Sogora huyo amewajibishwa na Man-City mara 168 na kuongoza waajiri wake hao kutwaa kila mojawapo ya mataji ya soka ya nyumbani tangu ajiunge nao kutoka Everton kwa kima cha Sh7.4 bilioni mnamo Agosti 2016.
“Navutiwa sana na kikosi hiki na nimejikuza zaidi kitaaluma tangu nisajiliwe na Man-City. Klabu hii inajivunia wanasoka wa haiba kubwa ambao wana malengo sawa na yangu – kuendelea kunyanyua mataji katika mashindano mbalimbali,” akasema Stones.
Ushirikiano mkubwa kati ya Stones na Dias katika safu ya ulinzi ya Man-City mnamo 2020-21, ni kiini cha kujumuishwa kwake katika Kikosi Bora cha PFA 2021.
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO