• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 5:50 AM
Haaland aokotea Dortmund pointi moja dhidi ya Cologne kwenye gozi la Bundesliga

Haaland aokotea Dortmund pointi moja dhidi ya Cologne kwenye gozi la Bundesliga

Na MASHIRIKA

FOWADI chipukizi raia wa Norway, Erling Braut Haaland, alifungia Borussia Dortmund bao la dakika ya mwisho na kusaidia waajiri wake hao kuambulia sare ya 2-2 dhidi ya Cologne katika Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga).

Haaland aliwafungulia Dortmund ukurasa wa mabao katika dakika ya tatu kabla ya Cologne kusawazisha kupitia kwa Ondrej Duda aliyefunga mkwaju wa penalti kunako dakika 35.

Penalti hiyo ya Cologne ilikuwa zao la mshambuliaji chipukizi raia wa Uingereza, Jude Bellingham kunawa mpira ndani ya kijisanduku chao.

Cologne waliokuwa wenyeji wa mechi hiyo walijiweka kifua mbele kupitia kwa Ismail Jakobs katika dakika ya 65 kabla ya Haaland kusawazisha mambo kwa kukamilisha krosi ya Ansgar Knauff na kuwavunia waajiri wake alama moja muhimu.

Matokeo hayo yalisaza Dortmund katika nafasi ya tano jedwalini kwa alama 43, nne nyuma ya Eintracht Frankfurt wanaoshikilia nafasi ya nne. Bayer Leverkusen wanasoma mgongo wa Dortmund kwa karibu sana kwa alama 40 katika nambari sita.

Haaland, 20, sasa amepachika wavuni jumla ya mabao 33 kutokana na mechi 31 ambazo amesakatia Dortmund hadi kufikia sasa msimu huu wa 2020-21.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Hatimaye mitihani yaanza kwa KCPE

Leicester waaibisha Manchester United na kufuzu kwa...