• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 2:31 PM
Inter Milan wapiga Atalanta na kufungua pengo la alama sita kileleni mwa jedwali la Serie A

Inter Milan wapiga Atalanta na kufungua pengo la alama sita kileleni mwa jedwali la Serie A

Na MASHIRIKA

INTER Milan waliwapokeza Atalanta kichapo cha 1-0 katika Ligi Kuu ya Italia (Serie A) mnamo Jumatatu usiku na kuweka wazi maazimio yao ya kutia kapuni ufalme wa kipute hicho muhula huu.

Bao la pekee na la ushindi katika mchuano huo lilipachikwa wavuni na Milan Skriniar aliyechuma nafuu kutokana na utepetevu wa mabeki wa Atalanta katika dakika ya 54.

Licha ya goli hilo kuwazindua Atalanta waliovamia lango la wenyeji wao takriban kila dakika katika kipindi cha pili cha mchezo, Inter walisalia imara katika safu yao ya ulinzi.

Ushindi uliosajiliwa na kikosi hicho cha kocha Antonio Conte uliwadumisha kileleni mwa jedwali kwa alama 62, sita zaidi kuliko nambari mbili AC Milan.

Mabingwa watetezi wa Serie A, Juventus wanashikilia nafasi ya tatu kwa pointi 52, mbili zaidi kuliko AS Roma wanaofunga mduara wa nne-bora. Atalanta wanakamata nafasi ya tano kwa alama 49, mbili pekee mbele ya nambari sita Napoli.

Chini ya Conte, Inter kwa sasa wameshinda mechi saba zilizopita za Serie A kwa mfululizo, matokeo yanayowaweka pazuri kutwaa taji la msimu huu kwa mara ya kwanza tangu 2020.

Kichapo kutoka kwa Inter kilikomesha rekodi nzuri iliyoshuhudia Atalanta wakisajili ushindi kutokana na mfulululizo wa mechi nne za awali.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Madereva wa tuktuk Githurai waonyesha umoja kuboresha kazi...

Ronaldo atakuwa tegemeo letu dhidi ya FC Porto –...