• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 12:48 PM
Kocha Scott Parker aondoka Fulham na kuyoyomea Bournemouth

Kocha Scott Parker aondoka Fulham na kuyoyomea Bournemouth

Na MASHIRIKA

MKUFUNZI Scott Parker sasa atadhibiti mikoba ya Bournemouth kwa kipindi cha miaka mitatu baada ya kuagana na Fulham.

Kiungo huyo wa zamani wa Fulham alianza kudhibiti mikoba ya Fulham uwanjani Craven Cottage mnamo Februari 2019. Hata hivyo, alishindwa kuzuia kikosi hicho kuteremshwa ngazi kwenye kampeni za Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) hadi Ligi ya Daraja la Kwanza (Championship) mwishoni mwa msimu wa 2019-20.

Ingawa aliwaongoza Fulham kurejea EPL mnamo 2020-21 baada ya kushinda mchujo, kikosi hicho kilishushwa ngazi tena mwishoni mwa muhula huo.

“Safari yangu ya ukocha imekuwa na changamoto tele. Nadhani huu ndio wakati mwafaka wa kuondoka Fulham. Sasa maazimio yangu ni kukisuka upya kikosi cha Bournemouth na kujitahidi kurejea katika soka ya EPL,” akasema Parker.

Parker anaingia Bournemouth kujaza nafasi ya kocha Jonathan Woodgate aliyeagana na kikosi hicho mnamo Juni 27, 2021 baada ya mkataba wake kutamatika rasmi.

Wasaidizi wa Parker uwanjani Vitality watakuwa Matt Wells, mkufunzi wa makipa Rob Burch, mkuu wa matokeo Alastair Harris, mchanganuzi wa mechi Jonathan Hill na kocha wa viungo Charlie Moore. Hao wote wanaungana na Parker baada ya kuondoka Fulham.

Bournemouth almaarufu ‘The Cherries’, pia wamethibitisha kwamba Neil Moss, Stephen Purches, Simon Weatherstone na Steve Hard waliokuwa wasaidizi wa Woodgate pia wameondoka kambini mwao.

Bournemouth walizidiwa maarifa na Brentford kwenye mchujo wa kuingia EPL mwishoni mwa msimu wa 2020-21. Woodgate alianza kudhibiti mikoba ya kikosi hicho mnamo Februari 2021 baada ya mtangulizi wake Jason Tindall kutimuliwa baada ya miezi sita pekee.

TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO

You can share this post!

Uhispania waingia robo-fainali za Euro baada ya kuangusha...

Sergio Ramos apokea ofa kutoka Bayern Munich, PSG na...