• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:55 AM
Mwanaspoti wa Safari Rally azikwa

Mwanaspoti wa Safari Rally azikwa

NA RICHARD MAOSI

MWENDESHAJI wa Safari Rally Arthur Kinyanjui ambaye alikuwa akitambulika kwa jina la utani kama AK47, alizikwa jana nyumbani kwao Bahati kaunti ya Nakuru.

Kinyanjui alikuwa amelazwa katika hospitali ya Aga Khan jijini Mombasa alipokuwa akiendelea kupokea matibabu mpaka alipopoteza maisha yake mapema wiki iliyopita.

Taifa Leo Dijitali ilitembelea nyumbani kwao eneo la Bahati Nakuru, na kushuhudia mazishi ambapo, viongozi kadhaa akiwemo makamu wa rais , Dkt William Samoei Ruto

alihudhuria.

Hatimaye marehemu alipumzishwa katika boma la wazazi wake.

Kulingana na msemaji wa familia, Kinyanjui alikuwa ni mwanamichezo shupavu wa kuyaendesha magari ya Safari Rally, na aliwahi kutamba ndani na nje ya Kenya.

“Marehemu aliletea taifa sifa nyingi, na hivyo basi ameacha pengo kubwa katika jumuia ya wanamichezo,”akasema.

Katika umri mdogo Kinyanjui alikuwa akiendesha gari aina ya Subaru Imprezza WRX, dhidi ya madereva mahiri kama vile Ian Duncun kwenye Mashindano ya Kimataifa ya Kenya National Autocross Championship(KNAC).

Aidha mnano mwaka wa 2009 alikuwa wa tatu kwenye mashindano ya Safari Rally, hatimaye miaka miwili baadaye alishiriki kwenye mashindano ya KCB Safari Rally na kufanya vyema.

“Februari mwaka huu Naibu wa Rais Dkt William Samoei Ruto, akiandamana na wanasiasa wa mrengo wa Tangatanga walimtembelea Kinyanjui, akiendelea kutibiwa mjini Mombasa,”akasema.

Kinyanjui ambaye ni mtoto wa mbunge wa Bahati Kimani Ngunjiri alikuwa ni umri wa miaka 32.

Kupitia mtandao wake wa kijamii Ngunjiri alieleza huzuni yake, akisema kuwa hakuamini kuwa alikuwa amempoteza mtoto wake ambaye alikuwa ni kitinda mimba.

  • Tags

You can share this post!

Mbunge ajipata pabaya kwa kutaka kuzima wapenzi wa nje ya...

Corona: DP Ruto asitisha mikutano yake ya hadhara