Na MASHIRIKA
KIKOSI kitakachotegemewa na Ujerumani kwenye Olimpiki zijazo jijini Tokyo, Japan kuanzia Julai 22 kilijiondoa uwanjani zikiwa zimesalia dakika tano pekee kwa mechi ya kirafiki dhidi ya Honduras kukamilika mnamo Julai 16, 2021.
Hii ni baada ya beki wa Ujerumani, Jordan Torunarigha, 23, kurushiwa matusi na wapinzani kwa lengo la kumbagua kirangi.
Mechi hiyo ambayo ilichezwa bila mashabiki kwa vipindi viwili vya dakika 30 kila kimoja, haikurejelewa baada ya tukio hilo matokeo yakiwa bado 1-1.
Torunarigha kwa sasa ni mwanasoka wa kikosi cha Hertha Berlin cha Ligi Kuu ya Ujerumani (Bundesliga).
Honduras walijiweka kifua mbele katika kipindi cha kwanza kabla ya Ujerumani kusawazisha kupitia nyota Felix Uduokhai wa Augsburg katika kipindi cha pili.
Torunarigha alichezea Hertha Berlin ligini mara 14 mnamo 2020-21 na kusaidia kikosi hicho kuambulia nafasi ya 14 kwenye msimamo wa jedwali la Bundesliga.
Ujerumani watafungua kampeni zao za Olimpiki dhidi ya Brazil mnamo Julai 22 jijini Tokyo.
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO