• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 2:29 PM
ODONGO: Viongozi wa Pwani hawana nia ya kuungana kisiasa

ODONGO: Viongozi wa Pwani hawana nia ya kuungana kisiasa

Na CECIL ODONGO

WITO wa viongozi wa Pwani wa kuunda chama kimoja kufikia 2022 utakuwa kibarua kigumu kwa kuwa ni jambo ambalo huchipuka kila mara wanapohisi wamebaguliwa kwenye masuala ya kitaifa.

Lakini msukumo huo hutokemea eneo hilo linapomezwa na mawimbi ya kisiasa wanapounga mkono vigogo au wawaniaji wa urais kutoka maeneo mengine.

Wiki iliyopita, baadhi ya wabunge wa ODM kutoka Pwani walitishia kung’atuka chamani ifikiapo 2022, baada ya kinara wa ODM Raila Odinga na baadhi ya maseneta kuunga mfumo mpya wa Ugavi wa Mapato.

Mfumo huo ambao bado haujapitishwa na utarejeshwa bungeni kesho kujadiliwa zaidi, unalenga kupunguzia kaunti za Pwani mgao wa fedha za ugatuzi zinazopokea kutoka kwa serikali kuu.

Eneo la Pwani lilikuwa chimbuko la ugatuzi kwa kuwa aliyekuwa kigogo wa siasa za ukanda huo hayati Ronald Ngala, alipendekeza mfumo wa utawala majimbo utumike hata kabla ya Kenya kujinyakulia uhuru 1963.

Hii ndiyo sababu kuu ya viongozi wake kuja pamoja na kuungana kulinda maslahi ya raia wao kwa kupinga kupunguzwa kwa mgao kutoka serikali kuu.

Inashangaza kwamba viongozi wa Pwani hurudia suala la uundaji wa chama chao kila mara ilhali uchaguzi unapofika wanaunga mkono na kuwania viti kupitia vyama vingine.

Tabia hii ilianza zamani kwani waliokuwa vigogo wa siasa za Pwani Marehemu Sharif Nassir na Karisa Maitha walielekeza kura za Wapwani kwa uongozi wa Kanu na Narc.

Baada ya kifo cha Bw Maitha mnamo 2004, waziri wa sasa wa Utalii Najib Balala alikuwa mwenge wa Pwani katika chama cha ODM kutoka 2007-2012 kabla Gavana wa Mombasa Hassan Joho kuchukua usukani waziri huyo alipohamia Jubilee mnamo 2013.

Kwa kifupi, chama cha ODM kina umaarufu Pwani huku baadhi ya vyama vilivyoundwa kushughulikia maslahi ya Pwani na kuwaunganisha vikikosa kushabikiwa na raia.

Vyama kama Shirikisho, Kaddu-Asili, USPPK, DPK na NLP viliundwa kwa kusudi la kuwaleta Wapwani pamoja lakini vikakosa kushamiri.

Hii ndiyo maana wabunge Aisha Jumwa (Malindi) na Owen Baya wa Kilifi kati ya wengine huenda wasitimize ndoto ya Pwani kuwa na chama kimoja hata kama mfumo mpya wa ugavi wa mapato utapitishwa bungeniKinachotia doa zaidi kwenye mpango wao ni kimya cha Bw Joho na Gavana Amason Kingi wa Kilifi kuhusu suala hilo.

Hii ni kwa kuwa wawili hao ndio wanaonekana kuwa wasemaji wa Wapwani kwa sasa.Ingawa ni haki ya kidemokrasia kwa kila kiongozi kuzungumzia suala analohisi linabagua jamii yake, bado viongozi wa Pwani wana kibarua kigumu kuzima migawanyiko na kuungana chini ya chama kimoja.

Kilicho wazi ni kuwa siasa kuhusumfumo wa ugavi wa mapato utakaopunguza mgao kwa kaunti za Pwani hazitoshi kuwashawishi wakazi kutema ODM na kuungana chini ya chama kimoja.

You can share this post!

2022: Ford-Kenya yamkemea Eugene

MATHEKA: Serikali yazidi kuvuruga Katiba, kuleta udikteta

adminleo