• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 7:47 PM
TAHARIRI: Makanisa mengine nao waige mfano kanisa la ACK

TAHARIRI: Makanisa mengine nao waige mfano kanisa la ACK

NA MHARIRI

MSIMU wa siasa huwa muda wa wanasiasa kufanya lolote. Ndio wakati ambao utawaona masokoni, matangani, harusini, na hata makanisani.

Kutokana na kanuni za kuzuia maambukizi ya corona, serikali ilipiga marufuku mikusanyiko ya watu kwenye viwanja na kumbi mbalimbali.

Maeneo pekee ambako bado watu wanapatikana kwa wingi, ni katika makanisa.Si ajabu kwamba ghafla wanasiasa wanaomezea mate kumrithi Rais Uhuru Kenyatta mwaka ujao, wamekuwa waumini wakuu kila Jumapili.

Jana Kinara wa chama cha ODM, Raila Odinga na mwenzake wa Amani National Congress (ANC), Musalia Mudavadi walikuwa kanisani Butere, Kakamega.

Kanisa la Kianglikana (ACK) lilikuwa likimtawaza Askofu wa Dayosisi ya Butere, Rose Okeno.Ingawa hafla hiyo ilikuwa ya kihistoria kwa kuwa Bi Okeno ni mwanamke wa kwanza kuchukua wadhifa huo, kuhudhuria kwa wanasiasa hao kulikuwa na lengo tofauti.

Ndio maana Askofu Mkuu Jackson Ole Sapit alipotangaza kwamba hawangeruhusiwa kuhutubu, waliondoka mmoja baada ya mwengine.Kwa kawaida, wanasiasa huwa wanatumia mialiko katika hafla za makanisa na ibada zinazohudhuriwa na watu wengi, kuuza sera zao, hasa wakati huu wa kampeni za uchaguzi mkuu.

Vigogo hao wa kisiasa huwa wanaandamana na wabunge na madiwani, na hugeuza hafla za kidini kuwa mikutano ya kampeni za kisiasa.

Bila aibu wanasiasa wanapopokea vipaza sauti, husahau kuwa wako mahali patakatifu. Hugeuza fursa ya kuzungumza kuwa nashambulizi dhidi ya wapinzani wao.

Askofu Ole Sapit aliwaambia wazi wanasiasa kote nchini kwamba wasitarajie kupatiwa nafasi ya kuzungumza wakihudhuria ibada katika makanisa ya ACK.

Kwamba kila mmoja anakaribishwa kanisani, lakini altari ni ya viongozi wa kidini pekee.Msimamo huu wa Askofu Ole Sapit kwamba kanisa la Kianglikana (ACK) hakitawapa nafasi wanasiasa kuzungumza, ni mzuri. Unafaa kuungwa mkono na Wakenya wote.

Viongozi misikitini wamekuwa na msimamo huu tangu zamani. Hata uwe nani, unaswali kwenye mikeka kama watu wengine. Swala ikiisha, unaondoka na kuendelea na shughuli zako.Lakini wanasiasa wamekuwa wakiotea majukwaa ya makanisa kuongea.

Wangekuwa wanazungumza mambo ya kuwajenga raia kiuchumi na kimaendeleo, hakungekuwa na sababu ya kuwa na wasiwasi.

Wengi wakipewa nafasi ya kuzungumza, huonyesha wazi kuwa hawana sera. Badala ya kueleza ni vipi wanapanga kubadili maisha ya vijana, akina mama, wazee na watu wengine, huanza kushambulia wenzao na kuvuruga heshima ya madhabau. Tabia hii si katika makanisa pekee.

Wanasiasa wamekuwa wakiotea matanga. Badala ya kuwafariji waliofiwa, hugeuza matanga hayo kuwa majukwaa ya matusi na fitina. Kwa hivyo Wakenya wengine yafaa waige hatua zilizochukuliwa na ACK.

You can share this post!

WANTO WARUI: Wanafunzi walio katika shule za maeneo hatari...

Viongozi watangaza azma yao kuwania kiti cha ubunge Thika