• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
BENSON MATHEKA: Wakenya wamechoshwa na undumakuwili wa magavana

BENSON MATHEKA: Wakenya wamechoshwa na undumakuwili wa magavana

Na BENSON MATHEKA

HATUA ya magavana kukana makubaliano ambayo Wizara ya Afya iliafikiana na madaktari na maafisa wa kliniki ili wamalize mgomo wao, yadhihirisha kwamba wahudumu wa afya hawana mfumo thabiti wa kushughulikia matakwa yao.

Kulingana na magavana, Wizara ya Afya haikufaa kukubaliana na wahudumu hao warudi kazini bila kuhusisha serikali za kaunti. Kwa kile ambacho kinaonyesha ukosefu wa nia njema, magavana wanasema kwamba serikali za kaunti hazitaweza kutimiza yale ambayo wahudumu hao walikubaliana na wizara.

Inasikitisha kwamba badala ya kushukuru wizara kwa kusaidia kumaliza mgomo ambao umelemaza huduma katika hospitali za umma na kufanya wagonjwa kuteseka, magavana wanailaumu kwa kukubali kutimizia madaktari na maafisa wa kliniki matakwa yaliyowafanya kugoma.

Kauli ya magavana kwamba baadhi ya kaunti zilikuwa zimetimiza matakwa ya madaktari ilhali wanaendelea na mgomo, yaonyesha wakuu hao wa kaunti ndio chanzo cha migomo inayovuruga huduma za afya mara kwa mara nchini.

Badala ya kulaumu wizara kwa kukubali matakwa ya wahudumu hao, magavana wanafaa kufanya nayo mazungumzo kuelewa sababu za maafikiano hayo.

Pia kutafuta mbinu za kurekebisha makosa ambayo huenda yalitokea, badala ya kuyapuuza na kuwafuta kazi madaktari.Wizara iliamua kuketi chini na wahudumu hao wa afya ikifahamu kwamba huduma za afya zimegatuliwa.

Katiba inasema kwamba serikali ya kitaifa na za kaunti zinategemeana, kwa hivyo magavana hawafai kufanyia mzaha suala hili nzito linalohusu afya ya raia. Je, wizara inayofahamu kwamba huduma za afya zimegatuliwa inaweza kuzungumza na wahudumu bila ufahamu wa magavana? Ikiwa ilifanya hivyo, nia yake ilikuwa nini?

Je, magavana walizungumza na wizara kabla kutoa taarifa yao kuruka makubaliano ya kumaliza mgomo?Ikiwa mazungumzo yalifanyika, kwanini walitoa taarifa ya kulaumu wizara? Je, nini hatima ya madaktari waliokuwa wamegoma, baada ya magavana kukataa makubaliano ya kurudi kazini kati yao na wizara ya afya?

Ukweli ni kwamba hatua ya magavana inaweza kutumbukiza sekta ya afya katika mzozo mkubwa zaidi iwapo madaktari na maafisa wa kliniki wataendelea kugoma.Matokeo yatakuwa mabaya zaidi ikizingatiwa Wakenya wengi maskini hutegemea hospitali za umma kwa huduma za matibabu.

Labda wakati wa kurejesha huduma za afya kwa serikali ya kitaifa, kama wanavyopendekeza baadhi ya wataalamu, umewadia.Madhumuni ni kuepushia Wakenya mateso wanayopitia kila wakati wahudumu wa afya wanapogoma.

Ukweli ni kwamba sio madaktari wanaoumia huduma za afya zinapovurugika, ni Wakenya walalahoi.Magavana watafute mbinu za kurekebisha hali; si kuwafuta kazi wahudumu wa afya Wakenya wakiendelea kuteseka.

You can share this post!

Uchaguzi wa Nairobi wasitishwa tena

MAUYA OMAUYA: Usitarajie mabadiliko Kenya mwaka huu