• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 5:55 AM
Facebook yazima ujumbe wa Uhuru kwa Museveni

Facebook yazima ujumbe wa Uhuru kwa Museveni

Na MWANDISHI WETU

MTANDAO wa Facebook jana uliweka onyo kwenye ujumbe wa Rais Uhuru Kenyatta ukidai kwamba ulikuwa wa kupotosha.

Baada ya onyo hilo, Ikulu ya Nairobi ililazimika kufuta ujumbe huo ambao Rais Kenyatta alikuwa amempongeza mwenzake wa Uganda Yoweri Museveni kwa kushinda uchaguzi wa urais.

Kwenye ujumbe huo, Rais Kenyatta alieleza, kupitia ukurasa rasmi wa Ikulu katika Facebook, kwamba ‘ushindi wa Museveni ulidhihirisha kwamba raia wa Uganda wana imani na uongozi wake’.Ikitoa onyo kuhusu ujumbe huo, Facebook ilidai kwamba ulichunguzwa na kubainika ulikuwa feki.

“Ujumbe huo ulichunguzwa kwingine na wachunguzi huru na ikabainika ni feki,” lilisema onyo la Facebook.

Hatua hiyo ilijiri baada ya mpinzani mkuu wa Museveni, Robert Kyagulanyi anayefahamika kwa jina maarufu la kisanii kama Bobi Wine, ambaye aliibuka wa pili, kudai kwamba uchaguzi ulikumbwa na udaganyifu.

Bw Museveni ametawala Uganda kwa miaka 35 na ataongoza kwa kipindi cha miaka mingine mitano kufuatia ushindi wake kwenye uchaguzi wa Januari 14.Wine, ameahidi kwamba atathibitisha madai yake hivi karibuni.

Tume ya uchaguzi nchini Uganda ilitangaza kuwa Museveni alishinda kwa kura milioni 5.8 huku Wine akifuata kwa kura milioni 3.48.

Onyo la Facebook ni pigo maradufu kwa Rais Kenyatta ambaye alifunga na kufuta anwani zake za kibinafsi za mitandao ya kijamii miaka miwili iliyipota.

Baada ya kuzifuta alidai kwamba alifanya hivyo kwa kuwa watu wanatumia mitandao ya kijamii kueneza udaku na kumtusi.

You can share this post!

Museveni aahidi kujali zaidi maslahi ya maskini

Uhuru hawezi kunisaliti – Raila