• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 5:10 PM
Wakazi wa Kilifi walalamika kutembea kilomita 10 kutafuta maji

Wakazi wa Kilifi walalamika kutembea kilomita 10 kutafuta maji

MAUREEN ONGALA na ANTHONY KITIMO

WAKAZI wa Kaunti ya Kilifi wanalalamika kwamba wanaendelea kutozwa pesa na Kampuni ya Maji ya Mariakani (KIMAWASCO) ilhali wamekuwa wakitembea kwa zaidi ya kilomita 10 kutafuta bidhaa hiyo muhimu.

Hii ni licha ya kwamba, kampuni hiyo iliwasambazia maji kwenye maboma yao ambayo sasa hayana hata tone moja. Wakazi hao wa vijiji vya Kaptukuz, Ganze, Kaloleni na Magarini sasa wanahofia kuambukizwa magonjwa yanayotokana na uchafu kwa kuwa wanalazimika kuteka maji kwenye visima vya wazi ambavyo pia hutumika kuwanyeshwa mifugo.

Wakazi hao wanataka Kimawasco ikome kuwatoza Sh411 kwa mwezi kwa kuwa hawajapata maji kwa zaidi ya miezi minne.

“Tunalipia maji ilhali mifereji yetu ni mikavu kwa zaidi ya miezi minne. Kila mwezi wanatutumia bili ya Sh410 jambo ambalo halikubaliki kamwe. Kwa nini wanakusanya ada za kila mwezi ilhali maji hatuna?” akasema mkazi wa Kaptukus, Khadija Kadzo.

Wakazi hao walisema wanashuku kampuni chache zinazopatikana katika kaunti hiyo zimeelekeza maji kwao na kusababisha ukosefu huo.

“Tunatumia bomba moja pamoja na kampuni zinazopatikana hapa. Tumejaribu kurai wasimamizi wa kampuni hizi kutuachia maji hata kwa siku nne pekee kwa wiki lakini hawajali kwa sababu bomba hilo liko kwenye eneo kunakopatikana kampuni zao na hatuwezi kuwadhibiti,” akasema Mkurugenzi wa Kimawasco Hezekiah Mwaura.

“Madai kwamba baadhi ya kampuni zimeelekeza maji upande wao si ya kweli ila nitachunguza na usimamizi wetu upande wa Mariakani kubaini msingi wa madai hayo,” akaongeza.

Katika kijiji cha Bomani, Kaunti ndogo ya Magarini, wanawake hulazimika kupiga foleni ndefu na kukesha usiku wakiteka maji kutoka kwa visima vilivyochimbwa na wenyeji.

You can share this post!

Pigo Man-City na Leicester masogora tegemeo De Bruyne na...

Daraja lililoporomoka Ngoliba lakwamisha shughuli nyingi