• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 5:10 PM
Wazee Lamu washauri wanaume waache kutumia kiholela dawa za ashiki

Wazee Lamu washauri wanaume waache kutumia kiholela dawa za ashiki

Na KALUME KAZUNGU

WAZEE chini ya Baraza la Wazee Lamu wamewashauri vijana na wakongwe watumie njia za asili katika jitihada zao za kutafuta kuongeza nguvu au kuamsha hamu ya kufanya mapenzi badala ya kumeza kiholela vidonge vya kuamsha ashiki ambavyo baadaye vinasababisha madhara.

Wazee hao wameeleza kutamaushwa kwao na jinsi wanaume wanavyofariki kiholela kisha baadaye ikidaiwa walikuwa wametumia dawa hizo za kuongeza hisia za mapenzi.

Mwenyekiti wa Baraza la Wazee wa Lamu, Sharif Salim, alisema wakati umewadia kwa wanaume, hasa vijana kutafuta ushauri kutoka kwa wazee ili kufahamishwa mbinu za jadi na salama za kufuata katika harakati zao za kupiga jeki burudani wawapo na wapenzi wao.

Bw Salim aliwashauri wanaume kunywa supu na hata kula nyama ya pweza, mafuta na nyama ya kasa wa baharini, akisisitiza kuwa vyakula kama hivyo husaidia kuleta msisimko wa mahaba kitandani.

Pia aliwashauri vijana kuzingatia lishe bora, ikiwemo kula samaki kwa wingi katika mlo wao iwapo wanahitaji nguvu za kufanya mapenzi.

Mwenyekiti huyo wa Baraza la Wazee pia alitaja mitishamba kama vile kungumanga ya kusaga, unywaji wa kahawa tungu na vyakula vingine vya kiasili, ikiwemo mhogo na njugu kuwa miongoni mwa lishe ambayo vijana na wanaume wa umri mkubwa wanafaa kuzingatia ili waweze kuamsha hisia za kufanya mapenzi na kuwakidhi vilivyo wawapendao.

“Zamani na hata sasa sisi tumedhibiti nguvu zetu za kufanya mapenzi kwa kutumia njia za asili ambazo ni salama na za uhakika,” akasema Bw Salim.

Alisema ni vyema wazee kwa vijana kurejelea mbinu za jadi, ikiwemo kunywa supu ya pweza, kula mafuta na nyama ya kasa wa baharini, kutumia kungumanga ya kusaga, njugu na vyakula vinginevyo ambavyo ni salama kwa afya zao.

Naibu Katibu wa Baraza hilo, Abubakar Shelali alitaja utovu wa maadili na utandawazi kuwa miongoni mwa mambo yanayosukuma jamii kufanya mambo kinyume na jadi.

Alisema kinyume na awali ambapo watu walikuwa wakianza mapenzi wakiwa na umri mkubwa wa hadi miaka 30 na zaidi, ulimwengu wa sasa umewakengeusha watu kiasi kwamba mtoto wa umri wa miaka 12 au 13 tayari anashiriki mapenzi na mwenzake wa jinsia tofauti.

Alisema hali hiyo imesababisha wanaume wa sasa kukosa nguvu wakiwa bado wadogo kiumri kutokana na kwamba tendo hilo la mahaba wamelianza mapema, hivyo kuishia kulikinai.

“Vijana wa sasa wanasukumika kutumia vidonge vya kuamsha hisia za mahaba kwani hisia hizo wanazikosa kutokana na kwamba wamekuwa wakifanya kwa muda mrefu tangia wakiwa na umri mdogo,” akasema Bw Shelali.

Wazee hao pia walitaja tabia limbukeni ya mipango mingi ya kando miongoni mwa wanaume kuwa mojawapo ya misukumo inayowafanya kuchukua hatua ya kumeza vidonge vya kuwasisimua ili kuwakidhi wapenzi wao wengi kwa wakati mmoja.

Mohamed Omar alisema anaamini iwapo watu watakuwa waaminifu katika ndoa zao, suala la wanaume kupatikana wamefariki kwa kumeza Viagra litapungua nchini na ulimwenguni.

Naye Mzee Kassim Shee aliwashauri wanaume wa sasa kuacha kuiga mambo wanayoona mitandaoni, ikiwemo picha na video za ngono na vinginevyo.

“Misukumo yote ambayo wanaume, hasa vijana wa sasa wanaishia kuifanya bila shaka wanaipata kwenye mitandao. Utamezaje vidonge vya kuamsha hamu ilhali hujaelekezwa na daktari kufanya hivyo? Lazima watu waache upotovu wa mitandao na wabaki na uhalisia wao,” akasema Bw Shee.

Matamshi ya wazee hao yanajiri wakati ambapo wataalamu wa afya nchini tayari wameonya wanaume dhidi ya kutumia vibaya vidonge vya kuamsha mahaba, ikiwemo viagra bila ya kufuata ushauri ama uelekezi wa madaktari.

Hii ni kufuatia visa kadhaa vilivyoripotiwa hivi majuzi hapa nchini na taifa jirani Tanzania na ulimwenguni kote kuhusiana na wanaume ambao inadaiwa wamefariki baada ya wao kutumia vidonge vya kuamsha hamu ya mahaba.

You can share this post!

Msihofu, tuko tayari kujaza nafasi za wakongwe Jelimo na...

Man-United wadengua Liverpool katika Kombe la FA na kufuzu...