• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 7:00 PM
Msihofu, tuko tayari kujaza nafasi za wakongwe Jelimo na Jepkosgei mita 800 – Moraa

Msihofu, tuko tayari kujaza nafasi za wakongwe Jelimo na Jepkosgei mita 800 – Moraa

Na AYUMBA AYODI

MALKIA wa mbio za kitaifa za mita 400, Mary Moraa amewataka makocha wasiwe na wasiwasi kuhusu uwezo wa Kenya kushindania medali za mbio za mita 800 baada ya magwiji Pamela Jelimo, Janeth Jepkosgei na Eunice Sum kuondoka.

Akizungumza baada ya kuweka kasi ya juu katika mbio za mita 800 kwenye msururu wa mbio za kupokezana vijiti za Shirikisho la Riadha Kenya (AK) wikendi, Moraa alisema kizazi kipya kikiongozwa naye kiko tayari kujaza mapengo hayo.

Moraa aliahidi Wakenya makubwa katika mbio za mita 800 mwaka 2021 akitupia jicho kufuzu kupeperusha bendera ya Kenya katika mbio hizo za mizunguko miwili kwenye Olimpiki jijini Tokyo, Japan mwezi Julai/Agosti.

“Ukweli ni kuwa naona niko na siku nzuri za usoni katika mbio za mita 800 kuliko za mita 400, lakini haimaanishi kuwa nitatupilia mbali kabisa mbio za mita 400. Nitashiriki mbio za mita 400 kujipima kasi,” alisema Moraa baada ya kukamilisha mbio za mita 800 katika nafasi ya kwanza kwa muda wa dakika 2:04.92 uwanjani Nyayo. Alifuatwa unyounyo na Josephine Chelangat (2:05.11) na Emily Cherotich (2:05.95).

Moraa, 20, ambaye aliwakilisha Kenya katika mbio za mita 400 kwenye Riadha za Dunia 2019 mjini Doha, Qatar, alisema kuwa analenga kutwaa tiketi ya kushiriki Riadha za Dunia za mbio za kupokezana vijiti mjini Silesia, Poland katika kitengo cha 4×400 ama 2x2x400 zitakazofanyika Mei 1-2.

Raundi ya tatu na mwisho ya mbio za kupokezana vijiti za AK itaandaliwa ugani Nyayo mnamo Februari 6 kabla ya mchujo wa kitaifa kufanyika Machi 26-27.

“Ninachotamani sana ni kuwa na maandalizi mazuri ya mbio za mita 800. Kile naweza kueleza Wakenya nitegeeni tu! Nitajituma vilivyo kupata muda unaohitajika kufuzu na nitafanya makubwa kwenye Olimpiki za Tokyo, Mungu akipenda,” alisema Moraa ambaye alizoa medali ya fedha ya mbio za mita 400 kwenye Riadha za Dunia za makinda wasiozidi umri wa miaka 18 mwaka 2017.

“Najua makocha wetu wamejawa na hofu kuhusu maisha ya baadaye ya Kenya katika mbio za mita 800, lakini tuko tayari kujaza mapengo yaliyoachwa na magwiji kama Pamela Jelimo, Janeth Jepkosgei na Eunice Sum,” alisema Moraa akiwa amejaa imani. Moraa anajivunia muda wake bora kwenye mbio za mita 800 wa dakika 2:03.27.

Jelimo aliandikisha historia kwa kuwa Mkenya wa kwanza kunyakua taji la mbio za mita 800 kwenye Olimpiki mjini Beijing, Uchina mwaka 2008 na pia anashikilia rekodi ya kitaifa ya dakika 1:54.01.

Jepkosgei alizoa taji la dunia la mbio za mita 800 mjini Osaka, Japan mwaka 2007 naye Sum akatawala Riadha za Dunia mwaka 2013 mjini Moscow, Urusi.

Hapo Januari 23, Jeremiah Mutai aliibuka mshindi wa mbio za mita 800 kwa dakika 1:47.40 akifuatiwa na bingwa wa Jumuiya ya Madola Wycliffe Kinyamal (1:47.77) ambaye amerejea kwa kishindo baada ya kuwa mkekani na jeraha la mguu na maumivu ya mgongo.

Cornelius Tuwei (1:47.80) na bingwa wa dunia wa makinda mwaka 2016 Kumari Taki (1:48.03) walikamilisha mduara wa nne-bora katika kitengo cha wanaume.

Imetafsiriwa na Geoffrey Anene

You can share this post!

Seneta Mwaura aitaka serikali ijenge madarasa zaidi shule...

Wazee Lamu washauri wanaume waache kutumia kiholela dawa za...