• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 5:10 PM
Wanawake Kenya hulipa maradufu kupata huduma za M-Pesa ikilinganishwa na wanaume – Utafiti

Wanawake Kenya hulipa maradufu kupata huduma za M-Pesa ikilinganishwa na wanaume – Utafiti

NA FAUSTINE NGILA

Wanawake wa Kenya wanalipa mara dufu kuliko wanaume kupata huduma za pesa kwa njia ya simu, hii ni kulingana na data zilizotolewa majuzi na Shirika la Utafiti wa Malipo Kidijitali la Uingereza, Caribou Data.

Taarifa ya Shirika hilo, Payments System Design and the Financial Inclusion Gender Gap, inaeleza kwamba utafiti uliofanywa katika miji mikuu nchini Kenya umefichua jinsi wanawake wanatumia huduma za Kampuni tajika ya Mawasiliano Nchini – Safaricom kama vile M-Pesa, M-Shwari na Fuliza.

Aidha, utafiti huo umeonyesha kuna ‘ubaguzi’ wa kijinsia katika ada zinazotozwa, ikibainika wanawake wanalipa karibu Sh11 kusambaza au kupokea pesa, nao wanaume wakigharamika Sh7, kiwastani (Takwimu zilizojiri baada ya kukokotoa hesabu kwa mujibu wa data walizokusanya, wanawake na wanaume walivyokumbatia matumizi ya kidijitali kutuma na kutoa pesa).

“Kimsingi, inafikia kadri jumla ya Sh30 kila mwezi kwa wanawake, nao wanaume Sh16,” inaeleza data ya utafiti huo uliofadhiliwa na wakfu wa Bill na Melinda Gates.

Utafiti huo unaashiria kwamba wanawake hawajapigwa jeki kifedha, wakilazimika kutoa kiwango cha chini cha pesa, kikikadiriwa kuwa wastani wa Sh800.

Hilo linaashiria kwamba wanatozwa gharama ya juu ya ada, wakilinganishwa na wanaume na ambao hutuma au kupokea kiwango cha juu cha pesa, kupitia huduma za M-Pesa.

Kwa mfano, kwa sasa kutuma Sh800 ada ya Sh12 inatozwa sawa na asilimia 1.5, ikilinganishwa na kutuma Sh15, 000 ada inayotozwa ikiwa Sh97 (sawa na asilimia 0.64 ya kiwango hicho).

Kampuni ya Safaricom imekuwa ikitoza kuanzia ada ya Sh10 kutuma kati ya Sh101 – 500, kiwango cha ada ambacho kinabashiriwa kuwa ghali.

Wakati huohuo, watumizi wa huduma za Safaricom kusambaza pesa, hulipa ada ya kadri ya takriban asilimia 1.5 ya kiwango jumla cha pesa, wanawake wakionekana kugharamika zaidi wakilinganishwa na wanaume.

Mabaliko yalishuhudiwa Safaricom ilipotathmini kiwango cha ada inayotozwa kati ya Sh100 – 1, 000, Kenya ilipothibitisha kuwa mwenyeji wa janga la Covid-19, ambapo serikali ilihimiza wananchi kukumbatia usambazaji na upokeaji pesa kwa njia ya M-Pesa.

Miezi kadhaa mwaka uliopita, 2020, Safaricom ilifutilia kwa muda ada inayotozwa kutuma kiwango cha Sh1, 000 kurudi chini, japo kampuni hiyo ilikuwa ikitoza shughuli za kutoa.

Afueni hiyo hata hivyo iliondolewa Janauri 2021.

Licha ya mikopo inayotolewa na Safaricom kupitia apu ya Fuliza kuvutia wanaume kuliko wanawake, wanawake wameonekana kuikumbatia kwa kasi.

Fuliza ilizinduliwa Novemba 2018, takwimu za Safaricom zilizotolewa Novemba 2020 zikionyesha kima cha Sh830 milioni hukopwa kila siku.

Aidha, apu hiyo inaendelea kukumbatiwa, asilimia 21 ya wanawake na 26 wanaume wakiitumia, kulingana na takwimu za utafiti wa Caribou Data.

“Kwa mujibu wa utafiti tuliofanya, licha ya idadi ya chini ya wanawake waliokopa Fuliza, idadi ya wanaoikumbatia mara kwa mara ni ya juu ikilinganishwa na ya wanaume. Wanawake walifanya wastani wa huduma mara 4, kila moja ya Sh140, ikilinganishwa na wastani wa 1.6 wanaume, Sh80 kila moja,” inaeleza ripoti ya utafiti huo uliojumuisha zaidi ya wanaume na wanawake 1, 000.

Dhihirisho wanawake kukumbatia matumizi ya Fuliza, inaashiria uzinduzi wa huduma zingine za pesa kwa njia ya simu unaweza kuwasaidia kutatua ukosefu wa fedha wanaopitia.

Kulingana na Bi Roselyne Wanjiru, Mtafiti wa Masuala ya Fedha kutoka Shirika la Kesholabs, Nairobi, anahoji wanawake wengi wana majukumu ya malezi hivyo basi kiwango cha kutuma na kupokea pesa miongoni mwao ni cha chini kutokana na gharama inayowakodolea macho nyumbani.

“Wanaume hutumia kiwango cha juu cha pesa kwa familia zao na pia katika utekelezaji wa miradi ya maendeleo na kuwekeza. Isitoshe, wana nafasi bora kupata madaraka kazini na nafasi zingine kujiimarisha kifedha wakilinganishwa na wanawake,” mdau huyo anaiambia Taifa Leo Dijitali.

Anaendelea kueleza kwamba ni siku za hivi karibuni tu mwamko umeanza kushuhudiwa miongoni mwa wanawake, ambapo wamepata nafasi za hadhi ya juu serikalini na pia katika mashirika, nafasi ambazo zinawawezesha kupata donge nono.

“Kenya inapaswa kukumbatia usawa wa kijinsia katika utendakazi, wanaume na wanawake wapate mshahara au mapato yanayotoshana, ili wanawake waamke,” anafafanua.

Kulingana na Data ya Caribou, wanawake na wanaume wamehimizwa kutuma pesa zenye thamani chini ya Sh100 na ambayo haitozwi ada yoyote.

Asilimia 25 ya watumizi milioni 29 wa huduma za M-Pesa wametajwa kukwepa kutuma kiwango cha pesa kinachozidi Sh100.

Kampuni ya Safaricom, pia ina apu ya M-Shwari, inayosaidia wateja wake kuweka akiba kwa njia ya kidijitali na asilimia 19 ya wanaume wameikumbatia, kiwango chao kikiwa juu ya wanawake ambao wamewakilishwa na asilimia 14.

Alice Anangi, Mwanzilishi na Afisa Mkuu Mtendaji wa Shirika la Zeden Technologies, lililoko jijini Nairobi, anasema hali ngumu kiuchumi inayoshuhudiwa kwa sasa, imechangia wanawake kuwa katika hatari ya kukumbwa na umaskini wakilinganishwa na wanaume, hasa kutokana na dhana potovu ya umiliki wa raslimali na maamuzi katika ugavi.

“Tunashuhudia ubaguzi katika shughuli ya kusajili wanafunzi vyuoni, ndoa za mapema miongoni mwa wanawake na ukosefu wa hamasisho kuwajumuisha kwenye huduma za fedha kwa njia ya kidijitali. Hali kadhalika, utamaduni wa wanawake wafanye kozi zisizohitaji nguvu kama vile za kiteknolojia unawanyima fursa kupata kazi zenye mapato ya juu,” Bi Anangi anafafanua.

Utafiti huo pia umeonyesha, wanawake wanatumia simu za hadhi ya chini, chocheo ambalo ni kikwazo kupata huduma bora za fedha kwa njia ya simu.

Simu ya hadhi ya chini haina uwezo wala nafasi ya kutosha kuhifadhi apu muhimu, hususan zinazotoa huduma za mikopo.

“Idadi ya wanawake wanaomiliki simu zinazogharimu chini ya Sh20, 000 ni ya juu mno, huku zenye thamani zaidi ya kiwango hicho cha fedha zikimilikiwa na wanaume,” utafiti wa Caribou Data unaeleza.

Taswira hiyo kulingana na Bi Wanjiru inachangiwa na ukosefu wa hamasisho wanawake wainuliwe kifedha na kimaendeleo katika jamii.

Idadi kubwa ya wanawake waliohojiwa wanamiliki simu zenye thamani ya chini ya Sh10, 000 (sawa na asilimia 54), tafiti hizo zikiashiria asilimia 92 ya wanawake nchini wanamiliki simu za thamani ya chini ya Sh20, 000.

Ilibainika wanawake wenye simu ghali wamekumbatia huduma za utoaji na utumaji wa pesa mara kwa mara, kimsingi huduma za kifedha kidijitali.

“Tuligundua wanaomiliki simu za thamani ya juu (Sh20, 000) wanatekeleza huduma zenye thamani ya wastani jumla wa Sh1, 647 kwa mwezi, wakilinganishwa na wenye simu za hadhi ya chini, ambao kiwango chao kimesimaia Sh878 kwa mwezi,” utafiti huo unaelezea.

Kiwango cha utoaji na utumaji wa pesa, wanawake wenye simu ghali pia kimetajwa kuwa zaidi ya mara saba kwa mwezi, huku wanaomiliki za bei ya chini kikiwa mara nne pekee.

TAFSIRI: SAMMY WAWERU

You can share this post!

Nitamwambia Uhuru akutimue, Atwoli amtishia Kagwe

Utepetevu Kenya Power ulivyoiletea familia mahangaiko