• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 5:10 PM
Kituyi arejea nyumbani kusaka baraka za urais

Kituyi arejea nyumbani kusaka baraka za urais

ONYANGO K’ONYANGO na BRIAN OJAMAA

ALIYEKUWA Katibu Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa kuhusu Biashara na Maendeleo (UNCTAD) Mukhisa Kituyi amerejea nyumbani eneo la magharibi kusaka baraka za kuwania urais 2022.

Akiongea na wakazi mjini Kimilili Dkt Kituyi alisema safari yake ya kumrithi Rais Uhuru Kenyatta kama rais wa tano wa Kenya imeng’oa nanga na “sitarudi nyuma”.

“Bunduki yangu ina bunduki moja ambayo inalenga Ikulu pekee na sitaangalia nyuma,” akasema huku akinadi kama kiongozi bora ambaye anaweza kuliongoza taifa hili.

Kituyi ambaye alihudumu kama Mbunge wa Kimilili kwa mihula mitatu kuanzia 1992 hadi 2007 alisema atatumia tajriba aliyopata katika ngazi ya kimataifa kuinua uchumi wa Kenya.

“Niko tayari kuongoza Kenya ili iweze kufikia upeo wa juu kimaendeleo. Nitaweza kufikia hili kutokana na tajriba yangu ya miaka mingi kama waziri serikalini na katibu mkuu wa UNCTAD ambalo ni asasi ya kimataifa,” akasema.

Dkt Kituyi ambaye amewahi kuwa Waziri wa Biashara katika utawala wa Rais Mstaafu Mwai Kibaki, alisema aliamua kurejesha nyumbani “kupata baraka kwa watu wetu kabla ya kuanza kampeni rasmi ya urais.”

“Ukitafuta kiti kama cha urais utahitaji kuzunguka kote nchini. Lakini unapofanya hivyo wananchi watakuuliza ikiwa una uungwaji mkono kutoka nyumbani kwenu,” akasema.

Kwa hivyo Dkt Kituyi aliwasihi wakazi wa eneo la magharibi wamuunge mkono ili aweze kupata uungwaji mkono kutoka maeneo mengine ya nchi.

Msafara mkubwa wa magari ulimsindikiza Dkt Kituyi kutoka uwanja mdogo wa ndege wa Matulo, eneo bunge la Webuye Magharibi. Alihutubia mikutano katika maeneo ya Ligulu, Misikhu, Kimilili, Kamukunywa na hatimaye nyumbani kwake Mbakalo katika eneo bunge la Tongaren.

Dkt Kituyi pia alifichua kuwa anafanya mazungumzo na vigogo kadhaa wa kisiasa, akitoa mfano wa mkutano kati yake na kiongozi wa ODM Raila Odinga na Seneta wa Siaya James Orengo.

“Juzi nilikutana na Raila, Orengo, na Profesa Kivutha Kibwana na kuwasihi waniunge mkono katika safari hii ya kukomboa nchi kwa sababu ni marafiki zangu wa enzi wa ukombozi wa pili,” akasema.

Hata hivyo, ni Profesa Kibwana, ambaye ni Gavana wa Makueni, aliyepata nafasi ya kuhudhuria hafla ya Jumamosi Bungoma. Bw Odinga, Orengo, Kituyi na Kibwana ni miongoni mwa wanaharakati waliopigania ukombozi wa pili mapema miaka ya 1990s wakishinikiza kurejeshwa kwa mfumo wa utawala wa vyama vingi.

Hata hivyo, hatua ya Dkt Kituyi kuwania urais imesawiriwa kama itakayovuruga ndoto za kiongozi wa ANC Musalia Mudavadi na mwenzake wa Ford Kenya ambao pia wametangaza azma ya kuwania urais 2022.

Tafsiri: CHARLES WASONGA

You can share this post!

Wabunge wandani wa Ruto wapokonywa walinzi, bunduki

Duka la Nakumatt linavyohudumia wateja kisiri Nairobi