• Nairobi
  • Last Updated April 26th, 2024 5:10 PM
UDA yaelekeza macho yake 2022 baada ya London

UDA yaelekeza macho yake 2022 baada ya London

ERIC MATARA na CHARLES WANYORO

WANDANI wa Naibu Rais William Ruto katika eneo la Bonde la Ufa sasa wanaamini kwamba chama cha UDA ndicho kitashinda kiti cha Urais 2022 baada ya kushinda uchaguzi mdogo wa wadi ya London.

Mwaniaji wa wadi ya UDA alizoa kura 1,707 na kumshinda mgombeaji wa chama cha Jubilee Francis Njotoge ambaye alipata kura 1,385.

Ushindi wa UDA sasa umeibua mashindano makali ya kisiasa kati ya chama hicho kipya na vyama vingine kama Kanu na Jubilee katika eneo la Kati nchi inapojiandaa kwa uchaguzi wa 2022.

“Naibu Rais na wandani wake walikuwa wakijaribu kuona iwapo chama hicho kimejizolea umaarufu wa kisiasa miezi michache baada ya kubuniwa. Hii ndiyo maana walidhamini mwaniaji na ushindi huo unawapa nguvu zaidi,” akasema mchanganuzi wa masuala ya kisiasa na wakili Steve Kabita.

Diwani wa wadi ya Kabazi Dkt Petet Mbae alisema ushindi wa UDA ni ishara tosha kwamba umaarufu wa Jubilee unaendelea kufifia na si kipenzi cha raia katika eneo la Bonde la Ufa.

“Ushindi huo umeonyesha kwamba UDA ni chama kitakachokuwa na umaarufu mkubwa hasa katika Bonde la Ufa kuelekea 2022,” akasema Dkt Mbae.

Lakini Katibu Mkuu wa Jubilee eneo hilo Peter Cheruiyot anasema bado Jubilee bado ni maarufu Nakuru na kote Rift Valley. Kwamba ushindi katika wadi moja haufai kuchukuliwa kuwa mizani ya kupima umaarufu wa chama hicho.

“Mwaniaji wa Jubilee alishinda kule Hell’s Gate na katika wadi ya London tulishindwa kwa kura chache mno ambazo ni karibu 200,” akatetea Bw Cheruyoit.

Hata hivyo, alikiri kwamba chama cha Jubilee kina kibarua cha kuweka mikakati ya kujiongezea umaarufu ili kisipitwe na UDA.

Uchaguzi mdogo katika wadi ya London ulionekana kuwa ubabe kati ya Rais Kenyatta na Naibu Rais ambaye alikuwa akimpigia upatu mwaniaji wa UDA. Siasa za BBI na 2022 zilitawala kampeni za uchaguzi huo mdogo.

Seneta wa Nakuru Susan Kihika aliwashukuru wapigakura wa wadi ya London kwa kuvumilia kuhangaishwa na vyombo vya usalama kisha kudhihirisha kuwa Naibu Rais ana ushawishi mkubwa eneo hilo.

Mbunge wa Kuresoi Kusini Joseph Tonui naye alisema kuwa UDA ndicho chama ambacho wakazi wengi wa Nakuru na Bonde la Ufa watakumbatia katika uchaguzi wa 2022.

Akizungumza katika eneobunge la Igembe ya Kati Kaunti ya Meru, Naibu Rais Dkt William Ruto alisema kuwa kuna mpango wa kuiba kura katika uchaguzi mkuu wa 2022 na serikali inapanga kuwatumia polisi kuwatatiza wagombeaji maarufu.

Dkt Ruto alisema Wakenya wana haki ya kujiunga na chama chochote cha kisiasa na wanafaa waruhusiwe kuwachagua viongozi wanaowapenda.

“Kuna watu ambao hawana manifesto na sasa wanapanga watumie nguvu na ghasia ili kuwalazimishia Wakenya viongozi. Polisi wetu hawafai waruhusu wanasiasa wawatumie,” akasema Dkt Ruto.

“Vijana pia hawafai kukubali kutumiwa na baadhi ya wanasiasa. Tunataka kila mwananchi aruhusiwe kumchagua kiongozi anayempenda. Siasa za chuki hazifai hapa nchini,” akaongeza.

Seneta wa Meru Mithika Linturi na wabunge John Paul Mwirigi (Igembe Kusini) Mugambi Rindikiri (Buuri) na Kirima Ngucine wa Imenti ya Kati nao waliwataka wakazi wa Meru wampigie Ruto kura 2022.

Naibu Rais alisema kuwa serikali yake itatoa Sh100 milioni kwa kila eneobunge nchini ili pesa hizo zitolewe kwa watu wa mapato ya chini ili kuwasaidia kuendeleza biashara zao.

You can share this post!

Fulham wawika ugenini na kuendeleza masaibu ya Liverpool...

Usalama: Masomo yatatizika Baringo