• Nairobi
  • Last Updated April 27th, 2024 5:55 AM
TAHARIRI: Spoti: Serikali iwazie miundomsingi zaidi

TAHARIRI: Spoti: Serikali iwazie miundomsingi zaidi

KITENGO CHA UHARIRI

HERI nusu shari kuliko shari kamili; hiyo ndiyo tamathali inayofaa kuambiwa serikali ya Jubilee.

Ni msemo unaohitaji kuzingatiwa katika masuala ya ukuzaji wa michezo nchini hasa kuhusiana na miundomsingi.

Serikali ya Rais Uhuru Kenyatta na naibu wake Dkt William Ruto, mnamo 2013 na 2017, kama njia ya kujipigia debe ili wachaguliwe katika nyadhifa hizo kuu, waliahidi wananchi makuu, yakiwemo yanayohusiana na viwanja na miundomsingi mbalimbali ya michezo.

Rais aliahidi kujenga angaa viwanja vitano vyenye hadhi ya kimataifa mbali na kujenga vingine vyenye hadhi kuu katika kila mojawapo ya kaunti 47 nchini.

Hali ilivyo sasa ni kwamba taifa hili linajivunia uwanja mmoja pekee wenye hadhi ya kimataifa ambao unaweza kutumiwa kuandaa mashindano ya kimataifa – uwanja huo ni Kasarani.

Uwanja mwingine wenye hadhi japo hauwezi kutumiwa kwa mashindano ya hadhi kubwa ni Nyayo.

Hivi ndivyo viwanja maarufu nchini. Kinaya kikuu ni kwamba ni viwanja vilivyojengwa zamani sana, katika enzi ya rais wa pili wa Kenya, marehemu Daniel Toroitich arap Moi.

Katika enzi ya Rais Mstaafu Mwai Kibaki, kisha mrithi wake Rais Uhuru, hakuna uwanja wowote wa thamani uliojengwa.

Hiki kwa hakika ni kinaya kwa sababu uchumi wa Kenya katika enzi za watangulizi wa Rais Uhuru, ulikuwa chini.

Kwa sasa taifa hili lina bajeti ya takribani Sh3 trilioni ilhali linashindwa kujenga uwanja wowote wa ziada.

Kinachosikitisha hata zaidi ni kuwa mataifa yenye uchumi mdogo ukilinganisha na Kenya mathalani Rwanda na Tanzania, yanajivunia miundomsingi ya hadhi.

Inapozingatiwa kuwa Rais Uhuru anastaafu mwaka ujao wa 2022, inavunja moyo zaidi kuwa hata uwanja mmoja kati ya hivyo vitano alivyoahidi, haujajengwa. Ndiyo maana tunasema, heri nusu shari kuliko shari kamili.

Heri Rais angeisukuma serikali yake kujitahidi kujenga angaa uwanja mmoja wa hadhi hiyo. Kwa kufanya hivyo, ataeleweka kwa urahisi atakapotaja changamoto zilizomzuia kumudu ujenzi wa viwanja hivyo.

Naam, twafahamu kwamba serikali kadhaa za kaunti chini ya utawala wa Rais Uhuru zimejenga viwanja vya hadhi ya kujivunia.

Hata hivyo, itakuwa bora zaidi iwapo serikali kuu itajaliza juhudi za kaunti hizo kwa kuwapa Wakenya uwanja mmoja wenye thamani kubwa.

You can share this post!

FATAKI: Raha jipe mwenyewe dada, siache vigezo vya jamii...

Ruto ataka majibu kuhusu ulinzi wake