• Nairobi
  • Last Updated May 8th, 2024 3:41 PM
Ruto ataka majibu kuhusu ulinzi wake

Ruto ataka majibu kuhusu ulinzi wake

Na WANDERI KAMAU

NAIBU Rais William Ruto sasa anamtaka Inspekta Jenerali wa Polisi, Hilary Mutyambai kujibu maswali kuhusu hali zilizomfanya kuwabadilisha maafisa wa GSU waliokuwa wakilinda makazi yake katika mtaa wa Karen, Nairobi.

Kufuatia mabadiliko hayo Alhamisi, makazi ya Dkt Ruto sasa yatakuwa yakilindwa na maafisa wa Polisi wa Utawala (AP) kutoka Kitengo cha Kulinda Majengo ya Serikali.

Lakini kwenye barua aliyomwandikia Bw Mutyambai jana Ijumaa, Msimamizi Mkuu wa Wafanyakazi katika afisi ya Dkt Ruto, Balozi Ken Osinde, alisema afisi hiyo inataka maelezo kamili kuhusu kile kilichochangia mabadiliko hayo.

“Tunataka majibu kuhusu uhusiano wa mabadiliko hayo na kauli ambazo zimekuwa zikitolewa na baadhi ya watu kwamba Dkt Ruto hatakuwa debeni kwenye uchaguzi mkuu wa 2022. Je, ni makosa yapi maafisa wa GSU waliokuwa wakilinda makazi ya Dkt Ruto walifanya ili kubadilishwa? Huenda hizi ni njama za kuwatumia watu wanaojifanya kuwa polisi kufuatilia mienendo ya Dkt Ruto, ambazo maafisa hao walikataa kuunga mkono?” akauliza Bw Osinde kwenye barua hiyo.

Kutokana na hilo, alisema wamekataa mabadiliko hayo, kwani yalifanywa bila kuzingatiwa kwa taratibu zifaazo kisheria.

Vile vile, alisema wanataka maafisa hao kurejeshwa, ili kuendelea na majumuku yao ya awali.

Bw Osinde pia alisema Bw Mutyambai ndiye ataelekezewa lawama, ikiwa Dkt Ruto ama jamaa yake yeyote yule atakumbwa na mkosi wowote.

Kauli yake inajiri huku Idara ya Polisi ikiendelea kushikilia kuwa hatua hiyo ni “mabadiliko ya kawaida.”

Hali hiyo iliendelea kuzua hisia mseto Ijumaa, huku watu mbalimbali wakijitokeza kukosoa uamuzi huo.

Katika hali isiyo kawaida, Katibu Mkuu wa Chama cha Wafanyakazi (COTU), Bw Francis Atwoli, alikosoa mabadiliko hayo akiyataja kuwa yasiyofaa.

Kwenye taarifa, Bw Atwoli alisema kuwa licha ya tofauti za kisiasa zilizopo, usalama ni haki ya msingi ya kila Mkenya.

“Hatua hiyo haifai kwani huenda ikageuzwa kuwa kisingizio kwa mkosi wowote ambao huenda ukamkumba Dkt Ruto,” akasema.

Watu wengine ambao wamekosoa hatua hiyo ni maseneta Johnson Sakaja (Nairobi), Ledama Ole Kina (Narok) kati ya viongozi wengine.

You can share this post!

TAHARIRI: Spoti: Serikali iwazie miundomsingi zaidi

Sihitaji OKA 2022 – Raila