Na CHARLES WASONGA
WABUNGE na maseneta wa Azimio la Umoja One- Kenya sasa wanamtaka Naibu Rais Rigathi Gachagua kuandikisha taarifa kwa Idara ya Upelelezi wa Jinai (DCI) wakidai alimtishia maisha kiongozi wao Raila Odinga.
Viongozi hao walisema kuwa endapo “chochote kibaya” kitampata Bw Odinga kabla au siku ya Jumatatu Bw Gachagua na bosi wake Rais Wiliam Ruto ndio watalaumiwa.
“Hii ndio maana tunamtaka mkuu wa DCI amwamuru Gachagua aandikishe taarifa kwa kusema kuwa anayo “suluhu ya mwisho kwa Raila na familia ya Odinga,” Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna akasema kwenye kikao na wanahabari Alhamisi katika majengo ya bunge, Nairobi.
Bw Sifuna, ambaye alikuwa ameandama na wabunge kadha wa Azimio, alisema kuwa muungano umeingiwa na hofu “kuhusu usalama wa Raila” kufuatia matamshi ya Bw Gachagua.
Kwa upande wa Mbunge wa Likoni Mishi Mboko alisema Bw Odinga hafai kutishwa na wakuu serikalini akimtaja mwanasiasa huyo kama mzalendo na mtetezi sugu wa wanyonge.
“Raila ni mzaliwa wa nchi hii, yeye ni kiongozi wa taifa hili na amekuwa mstari wa mbele kutetea haki za wanyonge katika taifa hili kwa muda mrefu. Kwa hivyo, Rigathi au kiongozi yeyote wa Kenya Kwanza hana haki wa mamlaka ya kumtishia kwa namna yoyote,” akasema.
“Wale ambao wanasema eti watahakikisha kuwa watamaliza Raila wajue kwamba Wakenya wote watajitokeza Jumatatu kulalamikia gharama ya juu ya maisha na kudorora kwa shilingi ya Kenya ambayo sasa inabadilishwa kwa Sh140 kwa dola moja,” akaongeza.
Viongozi hao walikariri wito wao kwa Wakenya wajitokeza kwa wingi jijini Nairobi kushiriki maandamano ya amani kuishinikiza serikali kutekelezwa matakwa ya Azimio.
Kando na kupunguza gharama ya maisha na bei ya bidhaa za kimsingi, viongozi wa Azimio pia wanataka sava za Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) zifunguliwe “ili Wakenya wapate ukweli kuhusu wizi wa kura katika uchaguzi mkuu uliopita”.
Dakika chache baadaye, wabunge wa Kenya Kwanza wakiongozwa na kiongozi wa wengi Kimani Ichung’wa wakisema kuwa Bw Odinga ndiye chanzo cha shida ambazo analalamikia wakati huu.
“Raila ndiye sehemu ya shida zinazokumba taifa hili wakati huu. Alishangia maamuzi mabaya yalifanywa na serikali ya Jubilee. Alikaa kimya wakati wa sakata ya ruzuku, sakata ya KEMSA na wizi wa Sh6 bilioni katika shirika la mawasiliano la Telkon Kenya,” akasema Mbunge huyo wa Kikuyu.
Subscribe our newsletter to stay updated