SHANGAZI;
Nimekuwa na mpenzi kwa miezi kadhaa. Nataka kuonja asali lakini amenipa sharti ambalo limenifanya nishuku si mtu mzuri. Anasisitiza niwe nikimpa pesa kwa huduma hiyo. Hayo ni mapenzi?
Hayo si mapenzi, ni biashara. Shabaha ya mwanamke huyo ni pesa tu, hana haja na mapenzi. Ukishindwa kuitimiza ombi lake atakuacha atafute aliye tayari kutoboka pesa. Achana naye utafute mpenzi wa dhati.
Nina miaka 28. Nimezaa mtoto na mwanamume mpenzi wangu lakini hanisaidii kumlea. Nafikiria kumuacha nitafute mwingine kwa sababu nahisi hana mpango wowote kuhusu maisha yetu pamoja.
Huna sababu ya kudumisha uhusiano na mtu asiyewajibikia malezi ya mtoto wake. Mwambie wazi kuwa huoni maana ya kuendelea na uhusiano huo. Wewe bado ni mchanga, usiendelee kupoteza wakati wako.
Nimekuwa na mpenzi kwa miezi sita. Nampenda sana na ninaamini anaweza kuwa mke wangu. Lakini kuna dalili kwamba anaweza akaniacha hivi karibuni. Nifanye nini?
Sijui ni dalili gani umeona za kuonyesha kuwa mpenzi wako atakuacha. Pili, kumbuka kuwa mapenzi na ndoa ni hiari ya mtu binafsi. Kwa hivyo kuwa tayari kwa uamuzi wowote kutoka kwake.
Nina rafiki wa kiume ambaye hunifaa kwa hali na mali. Ana familia lakini anataka tuwe na mpango wa kando. Sitaki kumkosea mkewe lakini pia nataka kudumisha urafiki wetu. Nishauri.
Urafiki wa dhati haufai kuwa na masharti. Mwambie ukweli kwamba huwezi kukubali ombi lake kwa sababu unaheshimu ndoa yake. Ni heri kuvunja urafiki kuliko kuvunja ndoa.