• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 9:55 AM
Idadi ndogo ya wanaojiandikisha wawe wapigakura yashuhudiwa kwenye vituo mbalimbali

Idadi ndogo ya wanaojiandikisha wawe wapigakura yashuhudiwa kwenye vituo mbalimbali

Na SAMMYWAWERU

SIKU mbili baada ya Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) kuzindua rasmi shughuli ya kuwasajili wapigakura wapya, idadi ya wanaojitokeza ingali ya chini mno.

Jumatatu, Oktoba 4, IEBC ilizindua kuanza kwa shughuli hiyo ambapo inalenga kuandikisha wapigakura wapya milioni 7.2.

“Tunahimiza wale ambao hawajasajiliwa wajitokeze kwa wingi,” akasema Mwenyekiti wa IEBC, Bw Wafula Chebukati akiongoza uzinduzi huo katika Kaunti ya Nakuru.

Usajili wa wapigakura wapya unatekelezwa kote nchini, wale ambao wanataka kubadilisha vituo vya kupiga kura pia wakipewa fursa.

Kwa mujibu wa sajili ya IEBC 2017, Kenya ina wapigakura 19,611,423 waliojiandikisha.

Huku viongozi na wanasiasa wakihimiza wapigakura wapya kujisajili ili kushiriki chaguzi mkuu ujao wa 2022, idadi ya wanaojitokeza ingali ya chini.

Uchunguzi wa Taifa Leo umebaini kwamba katika maeneo kadhaa Nairobi na viunga vyake, makarani wa kuwasajili wapigakura wanashinda mchana kutwa wakisubiri watu kwa sababu wanaojitokeza ni wachache mno.

Kwa mfano, makarani eneo la Mirema, mtaa wa Zimmerman, Nairobi wanaonekana kutulia wakijishughulisha na simu kwa muda mrefu kwa kukosa watu wa kusajili.

Katika uchunguzi wetu, Jumanne kati ya saa tano asubuhi hadi saa saba mchana meza ya makarani hao ilisalia bila kupata mpigakura yeyote wa kujiandikisha.

Hali hiyo haikuwa tofauti na ya Roysambu na Carwash, maeneo yaliyoko Zimmerman.

“Idadi ya wanaojitokeza kujiandikisha ni ya chini mno,” akasema karani mmoja na aliyeomba kutochapisha jina lake kwa sababu haruhusiwi kuzungumza na vyombo vya habari.

Taswira ya mtaa huo, iliwiana na ile ya Githurai 44, Githurai 45, Kasarani na Mwiki.

Tabia ya Wakenya kuchelea kujitokeza kujiandikisha kama wapigakura siku za kwanza, inaashiria mazoea ambayo yamekuwa yakishuhudiwa miaka ya awali kukimbilia foleni muda unapokaribia kuisha.

Zoezi la mwaka huu linatekelezwa kwa muda wa siku 30.

IEBC hata hivyo inasema haina uhakika endapo itaongeza muda zaidi, kipindi hicho kikikamilika kwa sababu ya uhaba wa fedha kuendesha shughuli hiyo.

“Mgao tuliopata hautatosha kuzidisha siku 30 tulizopangia kuendeleza usajili wa wapigakura wapya,” akasema Prof Abdi Guliye, Kamishna wa IEBC.

Prof Guliye aidha alisema tume hiyo ina uhaba wa mashine za kuandikisha wapigakura, kila wadi ikipewa mitambo tatu pekee. Kenya ina jumla ya wadi 1,450.

You can share this post!

Buda aliyefumaniwa alipa Sh0.5m

Wanafunzi 20,000 waahidiwa vitambulisho