Na VALENTINE OBARA
GAVANA wa Kwale, Bw Salim Mvurya, amesisitiza kwamba naibu wake, Bi Fatuma Achani ndiye anastahili zaidi kumrithi ifikapo 2022.
Bw Mvurya, ambaye anahudumu kipindi chake cha pili ambacho ni cha mwisho kwa ugavana, amekuwa akitangaza wazi mpango wake wa kutaka kumpokeza fimbo ya uongozi naibu wake.
Akizungumza katika mazishi ya Askofu Morris Mwarandu jana, gavana huyo alisema ni Bi Achani pekee atakayeweza kuendeleza mafanikio ambayo kaunti hiyo imeshuhudia tangu 2013.
“Ni vile hapa ni mazishini sitaongea zaidi. Lakini Askofu aliniambia ‘muda wako unaisha ututayarishie ya mbele’. Naibu gavana ametayarishwa. Mnaona Tanzania hakujakuwa na msukosuko? Katika taasisi ni lazima watu watayarishwe,” akasema.
Wengine wanaoaminika kumezea mate kiti hicho ni Mbunge wa Lunga Lunga, Bw Khatib Mwashetani, aliyekuwa Mbunge wa Mtuga Chirau Mwakwere, na katibu wa Wizara ya Kilimo Hamadi Boga.
Wakati huo huo, gavana alitaka wakazi wa Kwale ambao wanapakana na Tanzania wajihadhari dhidi ya maambukizi ya virusi vya corona.