• Nairobi
  • Last Updated May 13th, 2024 6:55 AM
Mwamunga alihudumu enzi ya Kenyatta na Moi

Mwamunga alihudumu enzi ya Kenyatta na Moi

KWA HISANI YA KENYA YEAR BOOK

Eliud Timothy Mwamunga alikuwa mwanasiasa mtajika kutoka Pwani hata kabla ya Kenya kupata uhuru na baadaye alihudumu kwa miaka mingi kama Mbunge na Waziri.

Aliwahi kushikilia nyadhifa kadha za uwaziri katika serikali za Hayati Mzee Jomo Kenyatta na Rais mstaafu Daniel Moi.Katika eneo linalojulikana kama kaunti ya Taita Taveta kwa ujumla, Bw Mwamunga ndiye anashikilia rekodi ya mwanasiasa aliyewahi kuhudumu kama mbunge kwa miaka 20 mfululizo.

Weledi wa Bw Mwamunga katika ulingo wa siasa ulimwezesha kunawiri katika serikali za Kenyatta na Moi nyakati ambapo wanasiasa waliokuwa wakiendeleza siasa za makabiliano walizimwa kwa kutupwa gerezani, kupokonywa nyadhifa zao za uwaziri au kuondolewa bungeni kupitia wizi wa kura.

Pengine ni sifa hizo zilizomwezesha kunawiri kuliko wanasiasa wengine katika eneo la Taita na Pwani kwa ujumla. Kando hayo Bw Mwamunga alikuwa tajiri aliyemiliki vipande kadhaa vya ardhi katika Taita Taveta yenye mali asili kama vile madini, mimea ya kuuzwa (kama vile mkonge) na wanyamapori.

Mwamunga alizaliwa mnamo Julai 21, 1935 katika kijiji cha Ishamba kando ya Milima ya Taita.

Alilelewa katika eneo hilo ambalo lina utajiri mkubwa wa mali asili, kama vile madini ya ruby, mikonge, matunda (maembe) na wanyamapori kwa sababu Mbuga ya Kitaifa ya Tsavo iko karibu.

Alianza masomo yake katika Shule ya Msingi ya Ishamba, kisha akajiunga na Shule ya Upili ya Shimo la Tewa kwa kidato cha kwanza hadi kidato cha nne.

Baadaye aliitwa katika Shule ya Upili ya Alliance kusome kiwango cha A’ level (vidato vya tano na sita).

Aliendelea na elimu ya juu katika chuo kikuu cha Makerere kisha akajiunga na Chuo Kikuu cha Dar es Salam ambako alisomea shahada ya Uanasheria. Mnamo 1969, Bw Mwamunga, akiwa na umri wa miaka 34, alijitosa katika kinyang’anyiro cha kuwania kiti eneobunge la Taita Taveta.

Alisema kuwa alipata hamasa kutoka kwa aliyekuwa mpiganiaji uhuru kutoka Pwani, Ronald Ngala ambaye alikuwa mstari wa mbele kupambana dhidi ya unyanyasaji wa watu wa pwani.

Baada ya kushinda kiti cha ubunge, Mwamunga alitekeleza miradi kadhaa ya maendeleo, alijenga urafiki na wataalamu wa kilimo, wahifadhi wa wanyamapori, wachimba madini wa asili ya Kenya na mataifa ya kigeni ambao walichimba rasilimali katika wilaya hiyo.

Vilevile, Bw Mwamunga alijenga uhusiano wa kisiasa katika ngazi ya kitaifa. Mkakati huu ulimfaidi kwani ulimwezesha kuchaguliwa tena katika uchaguzi mkuu wa 1974.

Ni baada ya kushinda kiti cha ubunge kwa mara ya pili ambapo Hayati Mzee Jomo Kenyatta alimteua katika baraza lake la mawaziri kuwa Waziri wa Ustawi wa Maji.

Katika kipindi cha miaka miwili aliyohudumu katika wizara hiyo Mwamunga alianzisha miradi kadhaa katika iliyokuwa Wilaya ya Taita Taveta.

Miongoni mwa miradi hiyo ilikuwa uchimbaji mabwawa, usambazaji wa maji katika maeneo ya miji na miradi ya unyunyiziaji mashamba maji kupiga jeki sekta ya kilimo.

Mnamo 1976, Rais Kenyatta alimhamisha Bw Mwamunga hadi Wizara ya Biashara na Viwanda na nafasi yake ikapewa Dkt Gikonyo Kiano, Katika Wizara hii mpya Mwamunga alisaidia katika utayarishaji wa sera nyingi ambazo ziliunda mazingira mazuri kwa watu kutoka ng’ambo kuwekeza nchini katika nyanja ya biashara na viwanda.

Na huku akifuata nyayo za Makamu wa Rais na Waziri wa Masauala ya Ndani wakati huo Daniel Moi na Kiano (aliyekuwa waziri wa Biashara na Viwanda), Mwamunga aliendesha sera ya kuhakikisha kuwa biashara za humu nchini zinamilikiwa na kuendeshwa na wenyeji.

Hii ni kwa sababu sekta hiyo ilitawaliwa na Wazungu pamoja na Wahindi ambao walipiga kambi jijini Nairobi na miji mingine mikubwa nchini, huku wanyabiashara wa asili ya Kenya wakikoosa nafasi ya kunawiri.

Kupitia uungwaji mkono kutoka kwa Rais Kenyatta, Mwamunga alitoa ilani kwa Wahindi waliokuwa wakiendesha biashara katika maeneo ya mashambani kuhama. Walitakiwa kujikita jijini Nairobi na miji mingine mikuu nchini.

Mawimbi ya kisiasa yalianza kumgonga Mwamunga mwishoni mwa 1977 wakati wa uchaguzi wa iliyokuwa chama tawala, Kanu.

Alitofautiana na Katibu Mkuu wa chama hicho wakati huo Robert Matano alipokuwa akisimamia uchaguzi wa tawi la Mombasa ambapo John Mambo alichaguliwa kama mwenyekiti.

Alikatalia mbali ushauri wa Matano kwamba uchaguzi huo urudiwe kutokana na udanganyifu uliogunduliwa.

Lakini licha ya Mwamunga kukosana Katibu Mkuu wa Kanu, alifaulu kuhifadhi kiti chake cha ubunge katika uchaguzi mkuu wa 1979 baada ya eneobunge hilo kubadilishwa jina na kuitwa, Voi.

Katika uchaguzi huo, wa kwanza baada ya kifo cha Kenyatta, Mwamunga alizoa kura 8, 364 na kumshinda mpinzani wake wa karibu Kwaya Mwatibo aliyepata kura 2,699 pekee.

Mnamo Januari 1992 Mwamunga alishirikiana na Kibaki kuunda chama cha DP baada ya Katiba kufanyiwa mabadiliko kurejesha utawala wa vyama vingi mnamo Desemba 1991.

Mwamunga aliteuliwa kwa mwakilishi wa chama hicho eneo la Pwani.

 

  • Tags

You can share this post!

Kibonge wa Afrika Mashariki Mandonga mtukazi...

Ustadh Wallah bin Wallah: Sijawahi kutuzwa Kenya licha ya...

T L