• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 7:50 AM
Nimekuachia Mungu, Samidoh aambiwa na mke kwa sababu ya kuchepuka

Nimekuachia Mungu, Samidoh aambiwa na mke kwa sababu ya kuchepuka

NA SAMMY WAWERU

NDOA ya mwimbaji wa nyimbo za Mugithi, Samuel Muchoki maarufu kama Samidoh iko kwenye mizani.

Hii ni baada ya mke wa mwanamuziki huyo, Edday Nderitu kuandika kwenye ukurasa wake wa Facebook ujumbe anaokiri kupitia mahangaiko chungu nzima katika ndoa.

Wawili hao wameishi kwenye ndoa kwa miaka 15, na Edday amesema ‘hana lolote kuambia Mungu kuhusu Samidoh ila anamuachia Muumba wa Mbingu na Nchi’.

Muimbaji huyo wa nyimbo za Kikuyu, amekuwa kwenye uhusiano haramu na seneta maalum, Karen Nyamu wakiishia ‘kujaaliwa’ watoto wawili pamoja.

Samidoh ambaye pia ni askari, na Edday wana watoto watatu.

“Imekuwa ndoa ya miaka 15 iliyosheheni miinuko na mishuko, msingi wetu ukiwa wa chini ambapo kidogo tulichopata tuliridhika ila chini ya miaka 3 iliyopita imekuwa yenye uchungu,” Edday akaandika.

Samidoh na Karen wamekuwa wakionekana pamoja hadharani, licha ya wawili hao kulumbana seneta huyo wa chama cha UDA akianika mahusiano yao mitandaoni.

Mwanasiasa huyo anayejulikana kwa kukabiliana vilivyo na wafuasi wanaomkosoa mitandaoni, alifichua kwa mara ya kwanza kuwa kwenye uhusiano na Samidoh.

Edday anasema licha ya kusalia mke mwaminifu, Samidoh amemchukulia kuwa ‘bubu’ na kumdunisha, bila kusahau kumkosea heshima.

Mama huyo analalamika kwamba amekuwa gumzo la mitandao ya kijamii, na kushambuliwa na wachangiaji kufuatia sarakasi na vituko vya afisa huyo.

Kupitia chapisho la Edday, amesisitiza kwamba kamwe hatakubali kuwa kwenye ndoa ya wake wengi.

“Nimekusaidia kukuza talanta yako, na jambo nililokueleza awali na nitarudia tena – Sitakubali kulea watoto wangu katika ndoa ya wake wengi (polygamy) hasa na mwanamke aliyenipita umri kwa zaidi ya miak 10, asiye na adabu wala heshima kwa familia yangu,” akafafanua.

Kufuatia umaarufu wa Samidoh, amekuwa akipata mialiko tele ndani ya nchi na hata ng’ambo kutumbuiza mashabiki wake kwa nyimbo za Mugithi.

“Nimekuwa nikiambia Mungu kila siku anipe nguvu kukuombea, ila leo sina cha kumweleza kukuhusu. Umenichukua pamoja na wanangu na kunitumbukiza kwenye bahari la uchungu, utakumbuka siku ya leo,” Edday akaelezea.

Ujumbe huo unaoashiria mama na mke anayepitia mateso na kuuguza majeraha ya moyo, Edday alisema atasimama imara kupitia nguvu za maombi.

Aliutoa muda mfupi baada ya picha za Samidoh na wakili Karen kuonekana pamoja katika hafla majuzi, kufichuka na kusambaa mitandaoni.

ReplyReply allForward
  • Tags

You can share this post!

Afisi ya mkewe Mkuu wa mawaziri yafunguliwa rasmi

Mkono wa Rais Ruto katika Raila kufutwa

T L