• Nairobi
  • Last Updated April 28th, 2024 4:55 PM
NMS kuzindua mpango wa kusafisha jiji la Nairobi na viunga vyake mara moja kwa mwezi

NMS kuzindua mpango wa kusafisha jiji la Nairobi na viunga vyake mara moja kwa mwezi

COLLINS OMULO na SAMMY WAWERU

SHIRIKA la Kuimarisha na Kustawisha Huduma za Jiji la Nairobi (NMS) litazindua mpango wa kusafisha jiji na viunga vyake kila mwezi.

Mpango huo unatarajiwa kuzinduliwa mwezi ujao, Februari, hasa kusaidia kuondoa mrundiko wa taka ambazo zimeendelea kutapakaa katika baadhi ya sehemu jijini.

Vilevile NMS imetoa onyo kwa wakazi wenye mazoea kutupa taka kiholela kwamba watachukuliwa hatua kisheria.

Shughuli ya kuimarisha usafi jijini itatekelezwa katika kaunti zote ndogo, 17, Nairobi, Jumamosi ya kwanza kila mwezi.

Mpango huo unajiri wakati ambapo utupaji taka kiholela umeonekana kuongezeka, suala ambalo linazua hofu kwa wakazi na kusababisha maradhi yanayohusishwa na uchafu kama vile Kipindupindu.

Kaunti ya Nairobi inakadiriwa kuwa na watu milioni tano, idadi ambayo inakisiwa kwa siku ‘huachilia’ tani 3,000 ya taka, ongezeko kutoka tani 2, 500 hapo awali.

Kwa siku, NMS hukusanya tani 2, 500 za taka. Awali, serikali ya Kaunti ya Nairobi ilikuwa ikikusanya tani 1, 000 kwa siku.

“Hivi karibuni NMS itaanza usafishaji wa Nairobi, Jumamosi ya kwanza kila mwezi,” akasema Mkurugenzi Mkuu wa Shirika hilo, Meja Jenerali Mohammed Badi.

Wiki iliyopita, NMS ilizindua matrela manane yatakayokusanya taka eneo la Kamukunji na Eastleigh.

Jumla ya tani 15 za taka zilizotapakaa katika majengo ya watu maeneo hayo na pia kwenye majaa zilikusanywa.

Mwaka uliopita, 2020 Meja Badi alisema wakazi wa Nairobi watahitajika kufanya usafi wa mazingira wanayoishi kila mwezi, ambapo alipendekeza kila mkazi kutenga siku moja kwa minajili ya udumishaji wa usafi.

NMS inasubiri kupata mwelekeo wa bunge baada ya kuwasilisha hoja hiyo bungeni.

Mpango wa kushirikisha wakazi kusafisha jiji la Nairobi na viunga vyake si mgeni, ikikumbukwa kuwa aliyekuwa Gavana wa Nairobi, Mike Mbuvi Sonko mwaka wa 2018 alikuwa amezindua mradi wa aina hiyo.

Chini ya mradi Ng’arisha Jiji, serikali ya Bw Sonko ilikuwa ikiendesha shughuli za kukusanya taka Jumamosi ya kwanza kila mwezi, ila baada ya kuandamwa na sakata za matumizi mabaya ya ofisi na mamlaka na ufujaji wa mali ya umma, Desemba 2019, mradi huo ulisambaratika.

Mpango wa NMS pia unajiri wakati ambapo serikali ya kitaifa inaendeleza mradi wa Kazi Mtaani, uliozinduliwa 2020 baada ya mkurupuko wa janga la Covid-19 nchini.

Mradi huo unaotekeleza katika kila kaunti, unashirikisha kufanya usafi wa mazingira, ambapo vijana wanafyeka nyasi kandokando mwa barabara na njia mitaani, kuzoa taka, kuzibua mitaro ya majitaka, kati ya shughuli zinginezo za usafi.

Umeajiri zaidi ya vijana 250, 000 hasa walioathirika kwa kukosa kazi kipindi cha corona.

Mitaa mingi Nairobi, ikiwemo Kariobangi, Eastleigh, Dandora, Zimmerman, Githurai, Mathare, Kibra, kati ya mingineyo inaendelea kushuhudia utupaji wa taka kiholela.

Ni hatari katika usalama wa wakazi, hasa kutokana na mkurupuko wa magonjwa yanayohusishwa na uchafu.

Itakuwa busara ikiwa NMS pia itaangazia suala la majitaka, na ambayo yanazua hatari katika mingi ya mitaa Nairobi.

You can share this post!

Hellen Obiri alenga kuonyesha wapinzani kivumbi kwenye Mbio...

Kanisa la Glory OutReach Assembly lazingatia kuhubiri amani