Na CHARLES WASONGA
WATAALAMU wa uchumi wamesema wabunge wamekuwa sehemu ya matatizo ya kiuchumi yanayokumba Kenya kwa sasa.
Kulingana na mtaalamu wa uchumi, Kwame Owino, serikali ya Jubilee ilisaidiwa pakubwa na wabunge katika kutumbukiza Kenya katika lindi la madeni.
“Pia ni wazi kuwa baadhi ya maafisa wa serikali walificha ukweli kuhusu hali ilivyokuwa, ama walichochea ukopaji bila kujali hatari waliyokuwa wakiweka taifa. Jubilee na Bunge walikuwa wameweka taifa katika mkondo wa kuzama kufikia mwisho wa kipindi cha kwanza cha utawala wake. Inawezekana kuwa rahisi kulaumu handisheki na BBI lakini ukweli uko wazi,” akasema Bw Owino.
Kulingana na Mkurugenzi Mkuu wa shirika la International Center for Policy and Conflict, Ndung’u Wainaina, wabunge hawawezi kujinasua kutokana na lawama kuhusu matatizo ya kiuchumi nchini.
“Katiba ya Kenya (2010) iliwapa wabunge mamlaka ya kuamua viwango vya ushuru, kuidhinisha bajeti na matumizi, kuweka sheria za ukopaji madeni ya kitaifa na kusimamia matumizi ya pesa zilizokusanywa kutokana na ushuru,” akasema Bw Wainaina.