• Nairobi
  • Last Updated May 2nd, 2024 9:37 AM
SAUTI YA MKEREKETWA: Wizara sasa ifanye uamuzi imara kuhusu vitabu teule vya fasihi

SAUTI YA MKEREKETWA: Wizara sasa ifanye uamuzi imara kuhusu vitabu teule vya fasihi

Na HENRY INDINDI

MOJA katika mambo yaliyozua mijadala mikali katika siku za hivi majuzi ni kusuasua kwa uamuzi kuhusu kuteuliwa kwa ama ‘Nguu za Jadi’ au ‘Paradiso’ miongoni mwa vitabu vingine vilivyoteuliwa vya fasihi.

Yamkini, kulikosekana uwazi katika uamuzi uliofanyika na kusema la haki kufikia sasa, walimu wananunua chochote katika vitabu hivi kwa matumaini ya kuteuliwa kimojawavyo.

Haya yameisawiri serikali kama isiyo na uwezo wa kufanya uamuzi bora au pengine inayokosa uwazi katika uamuzi muhimu kama huu.

Kadri tunavyoendelea kuchukua muda mwingi kuteua kitabu kitakachofunzwa na kutahiniwa ndivyo tunavyowakanganya wazazi na wanafunzi.

Tunaonekana kukiri peupe kwamba kweli huwa na au kulikuwa na mchezo mchafu katika uteuzi huo wa vitabu.

Taswira inayojengwa miongoni mwa wazazi, walimu na wanafunzi wetu kulihusu hili inatuacha na maswali mengi kuhusu ikiwa kweli tuna nia na tunaweza kupambana na ufisadi nchini.

Kwamba imepita miezi hii yote bila kutumwa rasmi kwa barua ya kulielekeza taifa, wazazi, walimu na wanafunzi kuhusu vitabu vilivyoteuliwa, ni dhahiri kwamba kuna tatizo kuhusu jinsi tunavyoiendesha elimu yetu.

Tusipohimiza na kujikumbusha kuhusu uwazi na haki katika usimamizi wa elimu, tutatoa wapi ujasiri wa kuwahimiza wanafunzi katika shule zetu kuujenga umilisi huo? Tutakuwa tukiwaeleza nini kimsingi kuhusu haja ya uaminifu na uwazi katika utendakazi wao maishani?

Mwelekeo

Hivi leo ningekuwa waziri wa elimu, baada ya kubaini kwamba mchakato huo ulikuwa na walakini mahali, ningechukua hatua ya kimakusudi kuukita msimamo wa wizara kulihusu hilo.

Ni ama ningeagiza mchakato huo kurudiwa na kuuhakikishia uwazi au ningechukua vitabu kutoka kwa mashirika ya serikali vilivyoshiriki katika mchakato huo wa uteuzi na kuuzima mjadala huu kwa msimu mzima.

Haiwezekani kukaa kwa kipindi hiki chote bila mwelekeo imara kulihusu suala hili.Uamuzi wa kuchukua vitabu kutoka kwa mashirika ya serikali ungetokana na ukweli uliopo kwa sasa kwamba serikali hununua vitabu na kuwapa wanafunzi shuleni.

Itakuwa picha ya aina gani kwa serikali kugharimika kusambaza vitabu vya mashirika ya kibinafsi kwa pesa ambazo si ufadhili kutoka nje?

Ufadhili kutoka kwa mashirika ya nje ni raslimali za kuwafaa wote kwa hivyo ufadhili huo ni haki ya kila shirika na kila mwananchi.

Ni katika ufadhili kama huo tu ambapo serikali inaweza kusambaza vitabu kutoka kwa mashirika ya kibinafsi.

Vitabu vinavyosambazwa shuleni kama vya mfumo wa umilisi na utendaji (CBC) ni zao la ushirikiano na wafadhili na hii ni haki ya kila mmoja.

Lakini kuchukua pesa za serikali kununua vitabu kutoka kwa mashirika ya kibinafsi huku kukiwa na vitabu vya kutoka kwa mashirika ya serikali ni moja tu katika hatua za kuuendeleza uozo huo.

Vinginevyo, kwa vitabu vya fasihi na vya kiada ambavyo havina ufadhili kutoka nje, serikali ijiondoe katika mchakato huo na kuyaachia mashirika uwanja huru wa kufanya biashara.

You can share this post!

KINA CHA FIKIRA: Asilan usimchape na kumtesa punda...

Wabunge lawamani kwa hali mbovu ya uchumi