• Nairobi
  • Last Updated May 17th, 2024 6:50 AM
Wabunge wa ODM wakosoa ubomoaji wa Njiru

Wabunge wa ODM wakosoa ubomoaji wa Njiru

Na CHARLES WASONGA

WABUNGE watatu wa ODM wameisuta serikali kuhusiana na ubomoaji ambao ulitekelezwa wa makazi ya watu uliotekelezwa katika eneo la Njiru, Nairobi

Matingatinga yaliyodaiwa kuwa ya Idara ya Utoaji Huduma Jijini Nairobi (NMS) yalibomoa makazi ya watu katika kipande kimoja cha ardhi katika eneo hilo, ambacho inadaiwa kimejengwa katika ardhi ya serikali.

Wakiongea na wanahabari katika majengo ya bunge Ijumaa, wabunge T. J Kajwang’ (Ruaraka), Anthony Oluoch (Mathare) na Zuleikha Hassan (Mbunge Mwakilishi wa Wanawake Kwale) walitaja kitendo hicho kama cha kikatili na kinachoonyesha kuwa serikali haijali maslahi ya watu wanyonge.

Bila kutaja majina, wabunge hao watatu walidai kuwa familia ya afisa mmoja mmoja serikali ndio inayopania kutwaa ardhi hiyo ambako zaidi ya familia 5,000 zimeishi kwa miaka mingi. Ubomoaji huo ulitekelezwa mnamo Machi 27.

“Iweje kwamba wewe mtu mwenye mamlaka na tayari una ardhi kubwa unawashambulia watu wadogo na kubomoa nyumba zao kwa njia ya kikatili? Hii ni kinyume cha sheria ikizingatiwa kuwa watu hawa wameishi katika kipande hicho cha ardhi kwa zaidi ya miaka 20,” akasema Bw Kajwang’.

Mbunge huyo ambaye ni wakili alidai kuwa nia ya ubomoaji huo ni kujitajirisha watu fulani wala sio kukomboa ardhi ya serikali.

Kwa upande wake, Bw Oluoch alisema kwa ODM kuamua kufanya kazi na serikali ya Jubilee, haimaanishi kuwa “sisi kama wabunge wa upinzani hatujaacha wajibu wetu wa kukosoa maovu yanayotekelezwa na serikali.”

“Ikiwa unadhani kwamba kwa sababu tunashirikiana kisiasa unaweza kutunyamazisha umejidanganya. Ijulikane kwamba tungali sauti ya wananchi. Tutapinga kile ambacho ni kibaya tukiwa katika viti vya nyuma bungeni,” akasema mbunge huyo wa Mathare.

Wabunge hao walisema wakazi hao walifurushwa bila kupewa ilani inavyohitajika kisheria.

Bi Zuleikha aliitika maelezo kutoka kwa Wizara ya Masuala ya Ndani akisema “tunasikia kuwa agizo hilo la ubomoaji lilitoka huko.”

You can share this post!

Ombi la mawakili kwa kaimu Jaji Mkuu

Mbakaji kusalia gerezani