• Nairobi
  • Last Updated May 4th, 2024 10:55 AM
Wabunge wakiri IEBC imepungukiwa na fedha za uchaguzi

Wabunge wakiri IEBC imepungukiwa na fedha za uchaguzi

Na CHARLES WASONGA

SIKU chache baada ya Mwenyekiti wa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC) Wafula Chebukati kulalamikia kupungukiwa na fedha za kufadhili matayarisho ya uchaguzi mkuu ujao, bunge linaonekana kuingilia kati suala hilo.

Mnamo Jumatano, Septemba 29, 2021, Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge kuhusu Bajeti Kanini Kega alitangaza kuwa wanachama wa kamati yake na wale wa Kamati ya Haki na Masuala ya Sheria watakutana na makamishna wa tume hiyo kujadili suala hilo.

Alitoa tangazo hilo kwenye kikao na wanahabari baada ya kukutana na wanne kati ya makamishna saba wa IEBC wakiongozwa na Naibu Mwenyekiti Juliana Cherera.

“Tunakubali kwamba IEBC inakabiliwa na upungufu wa fedha za kuandaa uchaguzi mkuu. Hii ndio maana tumeafikiana na makamishna hawa walionitembelea kwamba tutakutana nao kuchambua bajeti hiyo kwa lengo la kuziba mapengo yaliyopo,” Bw Kega akawambia wanahabari afisini mwaka katika jumba la KICC baada ya kufanya mashauriano na makamishna hao.

“Ninaweza kuthibitisha kuwa katika mwaka wa kifedha uliopita tulitengea IEBC Sh10 bilioni na katika mwaka huu wa kifedha tume hii imetengewa Sh16 bilioni. Sasa inakabiliwa na upungufu wa Sh14 bilioni kutokana na bajeti yake ya Sh41 bilioni,” akeleza.

“Kwa hivyo, tumekubaliana kwamba tutafanya mkutano na makamishna hawa pamoja na wenzetu wa JLAC ili tujadili suala hili la bajeti na masuala yote yanayohusu matayarisho ya uchaguzi mkuu wa 2022. Mkutano huo utafanyika wiki ijao,” Bw Kega, ambaye ni Mbunge wa Kieni akaongeza.

Alisema kuwa katika mkutano huo ambao utafanyika Mombasa, IEBC itapata nafasi ya kuwafafanulia wabunge jinsi itakavyotumia bajeti ya Sh41 bilioni.

“Tukishawishika kuwa bajeti hiyo ina mantiki hatutasita kuiuliza Hazina ya Kitaifa iongezee IEBC fedha katika Bajeti ya kwanza ya ziada itakayowasilishwa mwishoni mwa Oktoba mwaka huu,” Bw Kega akaeleza.

Alisema kuwa haja kubwa ya bunge ni kuiwezesha IEBC kuendesha uchaguzi mkuu kwa njia huru, haki na itakayoaminika na wadau wote.

Wakati huo huo, baadhi ya wabunge wameisuta IEBC kwa kupandisha bajeti yake kupita kiasi bila sababu maalum.

Kiongozi wa wengi katika Bunge la Kitaifa Amos Kimunya alisema hali hiyo inaashiria ubadhirifu wa pesa za umma ihali tume hiyo inaweza kuendesha shughuli hiyo kwa kiasi cha chini cha fedha kuliko Sh40.9 bilioni.

“India hutumia kiasi kidogo cha fedha kuendesha uchaguzi ikilinganishwa na Kenya ilhali ina idadi kubwa ya wapiga kura. IEBC inatuchezea shere kwa kuweka bajeti kubwa kiasi hiki,” akasema Bw Kimunya ambaye ni Mbunge wa Kipipiri.

“Hatuwezi kutumia Sh40 bilioni kila baada ya miaka mitano kugharamia uchaguzi. Ina maana kuwa kuna dosari kubwa katika tume hii,” akasema.

Lakini Bw Chebukati ametumia majukwaa kadhaa kutetea bajeti hiyo ya Sh40.9 bilioni akisema fedha hizo zitaiwezesha IEBC kuendesha uchaguzi kwa kuzingatia masharti ya kuzuia kuenea kwa Covid-19.

“Bajeti hii itatuwezesha kuwa na wapiga kura 700 katika kila kituo cha kupigia kura kulingana na mahitaji ya sheria,” akaeleza.

You can share this post!

Uhuru awashusha hadhi mawaziri Charles Keter na Simon...

Tukipunguza bei ya mafuta tutalemewa kufadhili shughuli za...