NA COLLINS OMULO
WAKAZI wa Syokimau katika kaunti ya Machakos wamelalamikia ongezeko la kelele kutoka kwa vilabu 36 vya burudani vinavyoendeshwa biashara katika eneo hilo.
Chini ya mwavuli wa Muungano wa Wakazi wa Syokimau (SRA), wakazi hao wanataka hatua kali zichukuliwe dhidi ya wamiliki wa vilabu hivyo na maduka ya kuuza vileo kwa kuvunja sheria za kudhibiti kelele.
Katika barua aliyoandikia serikali ya kaunti ya Machakos mwenyekiti wa muungano huo John Mutinda alilalamika kuwa wakazi wengi wanakosa usingizi kutokana na kelele.
“Baadhi ya wanachama wetu wamelazimishwa kuhamia makazi mengine au kutumia tembe za kuleta usingizi,” akalalamika.
Bw Mutinda aliongeza kuwa baadhi ya vilabu hivyo vinaendesha biashara zao kuzidi muda uliowekwa.