Na MASHIRIKA
TAFSIRI NA: CHRIS ADUNGO
KIUNGO matata raia wa Uholanzi, Georginio Wijnaldum, 30, amejiunga rasmi na Paris Saint-Germain (PSG) ya Ufaransa kwa mkataba wa miaka mitatu.
Nyota huyo aliyehiari kutorefusha mkataba wake kambini mwa Liverpool anatua kambini mwa PSG licha ya kuhusishwa pakubwa na Barcelona ya Ligi Kuu ya Uhispania (La Liga).
“Nimejiunga na mojawapo ya klabu bora zaidi katika soka ya bara Ulaya na ningependa kuwa sehemu ya historia nzuri ya mafanikio ya kikosi hiki cha PSG,” akasema Wijnaldum aliyejiunga na Liverpool mnamo 2016 baada ya kuagana na Newcastle United kwa Sh3.5 bilioni.
PSG waliokamilisha kampeni za Ligi Kuu ya Ufaransa (Ligue 1) mnamo 2020-21, waliwasilisha ofa nono iliyomshawishi Wijnaldum kubadili mawazo yake na kutupilia mbali ofa ya Barcelona.
Kuwepo kwa kocha Mauricio Pochettino kambini mwa PSG pia inaaminika kuwa kishawishi kingine kikubwa. Wijnaldum aliwahi kusifia pakubwa mbinu za ukufunzi wa Pochettino hata kabla ya kujiunga na Liverpool.
Nyota huyo ni sehemu ya kikosi kitakachotegemewa na Uholanzi kwenye fainali zijazo za Euro na amechezea Liverpool mara 237 huku akiwasaidia kutia kapuni taji la Ligi Kuu ya Uingereza (EPL) na ufalme wa Klabu Bingwa Ulaya (UEFA).