• Nairobi
  • Last Updated May 3rd, 2024 8:50 AM
Polisi wazima krusedi ya Pasta Ezekiel mjini Kilifi

Polisi wazima krusedi ya Pasta Ezekiel mjini Kilifi

NA MAUREEN ONGALA

POLISI wametia breki krusedi kubwa ya mhubiri wa kanisa la New Life Prayer Centre and Church, Ezekiel Odero.

Pasta Ezekiel alikuwa amepanga kuwa na ibada katika shamba la Kwa Kenga Mupa kwenye makutano ya kwenda eneo la Basi katika barabara kuu ya Kilifi-Malindi kwa siku tano.

Kamanda wa polisi wa Kilifi Kaskazini Bw Kenneth Maina alisema kuwa hatua ya kumkataza Ezekiel kuendelea na ibada yake iliafikiwa kwani hakuwa amewafahamisha maafisa wa usalama kwa wakati unaofaa.

“Kwa kawaida ni lazima tujulishwe ndani ya muda wa saa 72 lakini hakufanya hivyo,” akasema Bw Maina.

Mkutano huo ulitarajiwa kuanza Jumatano wiki hii na kumalizika Jumapili.

Hata hivyo, Maina alisema kuwa Ezekiel ataruhusiwa kuendelea na ibada hiyo juma lijalo kwa siku hizo tano.

Tayari matayarisho ya ibada hiyo yalikuwa yamekamilika na vijana walikuwa wameezeka mahema na majukwaa ya kuhubiria.

Nyasi ilikuwa imefyekwa katika uwanja huo.

Washirika walikuwa wameanza kumiminika katika eneo hilo.

Siku ya Jumanne, Ezekiel aliwatangazia waumini wake kuwa mkutano huo haungeweza kuendelea akisema baadhi ya washirika wageni kutoka ng’ambo ambao walitaka kuhudhuria hawakuwa wamefika.

Aliwaahidi kuwa ibada hiyo itang’oa nanga mara tu washirika hao watakapofika.

Ilimlazimu kubomoa mahema na majukwaa hayo na Jumatano jioni, vijana walikuwa wanapakia kwenye lori ili kuyarudisha katika kanisa lake katika eneo la Mavueni.

  • Tags

You can share this post!

Mama mmoja Kwale asimulia jinsi mwanawe alivyopigwa kwa saa...

Mchango: Familia ya mtandaoni yampa mtangazaji Kimani...

T L